Monday, September 3, 2007

Zemkala, Machifu, Maembe na Usiku wa Umoja

na innocent munyuku

MKUSANYIKO wa muziki wa reggae, midundo ya ngoma za asili kutoka kwa kundi la Zemkala na Bagamoyo Pirits ni mambo yanayoanza kulitikiza jiji la Dar es Salaam kiasi cha wiki mbili zilizopita.

Pengine niseme kuwa mashabiki wa muziki wamezoea mkusanyiko kama huo kuwa kwenye matamasha maalumu na si mazoea ya kila wiki. Lakini sasa hilo limewezekana baada ya Umoja Entertainment kuanzisha Usiku wa Umoja unaofanyika kila Ijumaa kwenye Ukumbi wa Art Gallery Mbezi Beach jijini Dar es Salaam.

Ni usiku wa mseto wenye kila aina raha kwa mashabiki wa muziki. Naam ndivyo ulivyo kutokana na mchanganyiko wa vipaji wasanii wa aina mbalimbali. Kuanzia wataalamu wa reggae, ngoma za asili na Madj wenye ujuzi wa kuwarusha mashabiki kwa staili nyingine za muziki kwa mtindo wa disko.

Lakini ukiachana na muziki wa Dj, cha kufurahisha ni mkusanyiko wa vichwa vyenye ujuzi wa muziki. Hawa ndio wasanii halisi waliopikwa wakapikika na wamedhihirisha hilo katika ulimwengu wa medani hiyo katika kona nyingi za dunia.

Tuanze na kundi la Zemkala. Hawa ni vijana wananane waliojikusanya kwa nia ya kuzinadi ngoma za asili. Zemkala ni neno la Kiyao likiwa na maana ya maendeleo.

Lije jua au mvua Zemkala hawana masihara kwenye kazi na ndio maana katika Usiku wa Umoja huko Art Gallery mashabiki wanapagawa kwa staili yao ya uimbaji na uchezaji wa ngoma za asili.

Kundi hilo linawajumuisha Yuster Nyakachara, Havintishi Baraza, Fadhili Mkenda, Yusuf Chambuso, Maulid Mastir, Kasembe Ungani, Shabaan Mugado na Fred Saganda.

Unapopigwa wimbo wa Tuvine (Tucheze) waweza kudhani kuwa jukwaa linasambaratika muda huo kutokana na kishindo kikuu cha ngoma za vijana hao ambao hawajavuka umri wa miaka 30.

Katika onyesho la Ijumaa iliyopita wakati mwendesha shughuli alipotangaza kuwa Zemkala walikuwa wanajiandaa kuvamia jukwaa na midundo ya asili, baadhi ya mashabiki pengine kwa ile dhana ya kubeza muziki wa utamaduni walianza minongÕono ya kutoridhika.

Lakini baada ya kundi hilo kuanza kuonyesha umahiri wao, hapakuwa na kuangalia pembeni zaidi ya kuwakodolea macho wasanii hao na kuwasindikiza kwa vifijo na nderemo. Huo ukawa ushindi kwa Zemkala dhidi ya fikra potofu zinazojali muziki wa kigeni.

Kabla ya Zemkala, kulikuwa na onyesho kutoka kwa Bagamoyo Pirits linaloongozwa na msanii kinara Vitali Maembe ambaye Jumamosi hii anamalizia stashahada yake kwenye Chuo cha Sanaa cha Kimataifa cha Bagamoyo.

Kama ilivyotarajiwa, Maembe na kundi lake wakiwa na mtindo wao wa Motokaa, waliwakumbusha mashabiki uhondo wa kibao cha Sumu ya Teja na hivyo kuwateka nyoyo mashabiki.

Ukiachana na hao, wengine waliokamilisha Usiku wa Umoja ni kundi la reggae la Machifu. Kazi ya wasanii hawa kwa hakika iliwashangaza wengi kutokana na ukweli kwamba si kundi linalofanya mazoezi ya pamoja.

Kila mmoja yu katika pilika zake na ikifika siku ya onyesho kila muhusika hukumbatia majukumu yake jukwaani na si rahisi kujua kuwa hawako pamoja katika mazoezi ya kila siku.

Wanapoimba kibao cha Julia moja kwa moja kutoka jukwaani si rahisi kujua watu hawa hawana mazoezi ya muda mrefu katika maisha yao. Hukutana saa chache kabla ya onyesho.

Ni wanamapinduzi, waliojaa fikra za kumkomboa mtu Mweusi kutoka kwenye makucha ya watu wa Magharibi. Makucha ambayo kwa miaka mingi yameendelea kuwaumiza Waafrika kwa kisingizio cha ustaarabu.

Hawa ni wakombozi wanaotumia magitaa, vinanda na sauti zao katika kuwalaani mafisadi wanaendelea kuikandamiza nafsi ya mnyonge si ndani ya Afrika tu bali duniani kote kunakohubiriwa upendo.

Lakini nini hasa kiini cha kuleta Usiku wa Umoja? Mwasisi wa usiku huo, Gotta Warioba ameliambia gazeti hili kuwa lengo ni kuwapa mashabiki mseto wa burudani.

ÒHili wazo ni la muda na nimekuwa nikiwaza kuwa kuna umuhimu wa kuwa na kitu kama hiki kwa sababu bila mkusanyiko wa aina hii hatuwezi kufika mbali.

ÒUmekuwa shahidi hapa. Wasanii wamepiga reggae, ngoma za asili na huu ni mwanzo tu nadhani katika siku zijazo tutakuwa na ladha tofauti tofauti zaidi,Ó anasema Gotta.

Lakini mbali na kuwakusanya mashabiki kwa lengo la kuonyesha uwezo wao, Gotta anasema huo ni mwanya kwa vikundi kuendelea kuwa katika joto la jukwaa kila leo.

Anasema si jambo zuri kwa msanii kusubiri mialiko ya msimu wakati upo uwezo wa kuwakutanisha kila wiki. Kwamba mbali na kubadilishana mawazo, mkusanyiko kama huo ni sawa na kisima cha ujuzi kwa wasanii.

Je, wasanii wenyewe wanasemaje kuhusu Usiku wa Umoja? Maembe anaeleza kuwa amefarijika kutokana na utaratibu huo kwa sababu mbali na kujitangaza, wanapata fursa ya kuona mwamko wa mashabiki dhidi ya kazi za sanaa.

Kauli kama hiyo haina tofauti sana na Kasembe Ungani wa Zemkala. ÒTumekuwa tukisubiri sana mambo kama hayaÉhapa unazidi kuwa mwenye hamu ya kuendelea na sanaa kwa sababu unapata changamoto za kila aina.Ó

Lakini kwa mujibu wa Ungani changamoto pia kwa watu wengine wanaojitangaza kuwa wasanii wakati hawana ubunifu wowote.

ÒSisi hapa umeona tunapiga kazi moja kwa moja hakuna anayetumia CD kuimba, watu wanapiga vyombo kwa ubunifu mkubwa. Hii ndiyo tofauti na hao wengine,Ó anaeleza.

Anasema kutokana na hilo ni vema wanaodhani kuwa wasanii wakajipanga upya kwani kuimba pasipokujua upigaji wa ala mbalimbali na elimu ya muziki kwa ujumla ni kujidanganya.

Kwa mtazamo wangu, usiku huu usiwe kama mbio za sakafuni. Wasanii pamoja na waandaaji waendelee kulitangaza jina la sanaa kwa ubora unaosubiriwa na mashabiki.

Ni wazi kuwa kama mjumuiko wa aina hiyo utaendelea kuimarishwa, wasanii watakuwa na nafasi nzuri ya kujiimarisha katika kazi zao za kila siku kwani umoja daima ni nguvu.

Umoja una umuhimu mkubwa katika maisha ya mwanadamu na hilo limewekwa kwenye maandiko ya Biblia na Quran pia. Kwamba tuwe na umoja ili kujenga uhusiano mwema daima.

No comments: