Monday, September 3, 2007

Prof. Ishengoma: Si lazima wote twende bungeni

na innocent munyuku
NI asubuhi ya saa mbili na nusu hivi. Jumamosi iliyotulia, siku ambayo nimejaa shauku ya kukutana na msomi aliyebobea katika masuala ya kilimo lakini akaamua kuwania nafasi ya chini katika siasa.
Huyu si mwingine bali ni Profesa Romanus Ishengoma (54), Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine Morogoro ambaye hivi karibuni iliyopita amefanya mahojiano maalumu na RAI na kutoboa kisa cha yeye kujiingiza katika siasa akiwania nafasi ya chini kabisa.
Akiwa amevalia vazi la kaptula na shati la bluu ananifuata katika lango kuu la kuingilia nyumbani kwake eneo la Falkland mjini Morogoro. Ananikaribisha baada ya utambulisho mfupi. Ni mwingi wa mazungumzo lakini kila anachozungumza hasiti kukitolea mifano na wakati mwingine kukushirikisha katika mazungumzo kwa kuuliza maswali.
ÒUnaujua huu ni mti gani?Ó ananiuliza akinionyesha mti mmojawapo unaopendezesha nyumba yake iliyozungukwa na mti. Mti huo anaouliza ni wa aina ya cacao ambao kwa mazoea haulimwi nchini Tanzania.
Lakini baadaye ananieleza kuwa anaelewa fika kwamba si kwenda kuangalia miti aliyoipanda na hivyo ananipisha niendelee na kiini cha safari yangu.
Nami bila kusita namjibu kwamba kilichonileta ni habari ya miti pia kwa hiyo hana haja ya kuacha kuzungumzia suala la mazingira. Tunashirikiana kicheko na kuketi katika viti nje ya nyumba yake.
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana, wengi hawakuelewa pale waliposoma kwenye magazeti au kupata habari kupitia vyombo vingine kwamba Profesa wa Chuo Kikuu anawania nafasi ya udiwani wa Kata ya Mbuyuni mjini Morogoro.
Prof. Ishengoma analielezea jambo hilo kuwa ni msimamo wake katika maisha.
ÒSiwezi kuwa driven (kuendeshwa) na mkumbo, na hii ni kwa sababu nina elimu ambayo ndio msingi mkubwa wa maisha.
ÒKusema tu kwamba mimi ni profesa haitoshi, mchango wangu ni nini katika jamiiÉmaendeleo daima huanzia katika grass roots na huu ndio mchango,Ó anasema na kisha kuongeza:
ÒKwa hiyo unapozungumzia udiwani unazungumzia msingi wa mambo mengi ya jamii, na labda niwakumbushe wanaonishangaa kwamba udiwani hauniondelei uprofesa nilionao.Ó
Anasema aliona ni vema aanzie na udiwani kwani ipo haja ya kujenga msingi.
ÒNawashauri wasomi au niseme maprofesa wenzangu, tuache kulalamika na badala yake tuanze kuwaletea maendeleo wananchi sehemu tunazoishi.
ÒLakini hapa pia tuwekane sawa kwamba si lazima wote twende bungeni. Maprofesa wamebaki kulalamika na wengi hawataki kuwatumikia wananchi,Ó anasema.
Je, katika uchaguzi huo wa mwaka jana hakutengwa na wananchi wa Morogoro kwa ukabila hasa ikizingatiwa kwamba yeye ni mtu wa Bukoba?
ÒWananchi wa Morogoro si wakabila, naomba tusiwapakazie. Lakini niliwahi kusikia minongÕono juu ya jambo hilo. Lakini hawa mimi ni ndugu zangu.
ÒHili nalisema kwa uwazi kabisa, Waluguru ni ndugu zangu. Nimekaa hapa kwa miaka zaidi ya 30 na sioni kama natengwa kama wapo wenye hulka hiyo ni wachache. Sasa hatuwezi kusema Waluguru ni wakabila wakati wenye tabia hiyo si wengi.Ó
Anazungumziaje Serikali ya Rais Jakaya Kikwete hasa katika kipindi hiki cha kuelekea mwaka mmoja madarakani?
Prof. Ishengoma ambaye Januari 19 mwaka huu alichaguliwa kuwa Meya wa Manispaa ya Morogoro anasema Kikwete kaanza vizuri katika uongozi wake.
ÒHuu mwaka mmoja wa Kikwete vya kusifiwa ni vingi kuliko lawama, kuna kasi ya maendeleoÉkuna attitude ya uwajibikaji kwa viongozi.
ÒAmekuwa Rais ambaye hakai chini katika utendaji. Sasa kama Rais anakosa muda wa kupumzika wewe wa chini utalalaje?Ó anahoji Prof. Ishengoma.
Anasema pia katika nyanja za kiusalama, Serikali ya Kikwete imefanya jitihada na imefanikiwa kupunguza nguvu za ujambazi.ÒUsalama wa raia upo ingawa sehemu za Magharibi bado kuna tatizo.Ó
Lakini je, vipi kuhusu tatizo la umeme linalowakabili Watanzania na uchumi wao? Prof. Ishengoma anasema si jambo jema kumtupia lawama Rais Kikwete pekee.
ÒTusimtafute mchawi, hili suala la umeme lina uhusiano mkubwa na mazingira. Sisi tunazalisha umeme wa maji, watu wanaharibu mazingira unategemea nini?
ÒHatuna reserves za majiÉlazima tujifunze kutunza mazingira na hili si la kuzembea kabisa ni vizuri kuvisaidia vyanzo vya maji.
ÒMimi nipo Morogoro tangu mwaka 1973 wakati huo kulikuwa na maji yanatiririka milimani na hata marehemu Mbaraka Mwinshehe aliimba. Leo hii hakuna kitu kama hicho. Tuwajibike sasa kwa pamoja.Ó
Anapozungumzia suala la Tanzania kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki, anasema Watanzania hawana haja kuwa waoga na muungano huo.
ÒNi kweli tuna suala la Muungano wetu na Zanzibar ambalo linasumbua kidogo, lakini huwezi kukataa Jumuiya kwa kigezo cha Zanzibar.
ÒTunatakiwa kuelewa kuwa kuna mambo ya bed room (chumba cha kulala) na sitting room (sebuleni) sasa mazungumzo ya vyumba ni tofauti kabisa.
ÒKuleta hoja ya woga hapa huu ni ujinga na hatuwezi kusema kuwa hatuendi huko. Sisi kama nchi hatuwezi kukwepa mabadiliko. You change or changes will change you. Mimi naona tusisubiri mabadiliko yatubadilishe ni heri tubadilike sasa,Ó anasema na kuongeza:
ÒDunia inakwenda na wakati kwa njia ya muungano. Sasa kama dunia inaungana sisi tunasubiri nini?
ÒSuala hapa basi liwe ku-survive na tujiulize how do we join. Je, tunakubaliana nini huko? Tunafanyaje? Lakini isiletwe hoja ya kipuuzi kwamba tukwepe kuungana. Tutakwisha.Ó
Anaongeza kuwa jambo la msingi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ni kuangalia Tanzania inapeleka kitu gani sokoni. Anasema kwa mfano kama Wakenya wana uhaba wa mahindi ni jukumu la Watanzania kulima mahindi na kuyasambaza katika soko la Kenya.
ÒMbona leo hii tunakula apples za Afrika Kusini? Hapa sasa tuangalie nafasi yetu kisoko na si kukwepa muungano huu.Ó
Mbali na kuungwa kwake Jumuiya ya Afrika Mashariki, Prof. Ishengoma ni mtu wa karibu anayependa kuona wanawake wanapewa nafasi katika jamii.
Anasema si jambo jema kuwafungia wanawake kwenye chupa. ÒWape uhuru waonyeshe vipaji vyao na tuache dharau dhidi yao.Ó
Lakini kuna jambo jingine linalomkera sana. Nalo ni vijana kupotoka kimaadili. Anasema vijana wengi wanataka kuwa Wamarekani; hawautaki Utanzania.
ÒWako brain washed kabisa lakini wameharibiwa na sinema wanadhani kuwa hayo ndiyo maisha halisi. Vijana hawa ni kama kuku broilers, sisi tunataka kuku wa kienyeji.Ó
Katika maisha ya kawaida, Prof. Ishengoma ametumia elimu yake ya misitu kuyatengeneza mazingira ya makazi yake.
Kuna miti mbalimbali mojawapo ni cacao ambao wengi wanaamini kuwa miti hiyo haiwezi kustawi hapa nchini. Ana miti aina ya mdalasini, miembe na bwawa la samaki.
Kimsingi hakuna zao la bustani ambalo utalikosa kwa Prof. Ishengoma na anajivunia jambo hilo na kwamba amefanya hivyo kupunguza gharama za maisha.
ÒLitakuwa ni jambo la ajabu sana kama nitakwenda sokoni au mtu wa familia yangu anakwenda sokoni kutafuta nyanya, ndizi au pilipili. Nina kila kitu humu ndani,Ó anasema Prof. Ishengoma.
Profesa Ishengoma alizaliwa mkoani Kagera Aprili 4, 1952 alikopata elimu yake ya msingi kabla ya kujiunga na sekondari ya Nyakato mkoani Mwanza.
Alimaliza kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Mazengo mkoani Dodoma mwaka 1972 na mwaka uliofuata Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kampasi ya Morogoro ambayo baadaye ndiyo ilizaa SUA.
Mwaka 1986 alipata udaktari wa sayansi ya kilimo kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Norway na mwaka 1996 akawa profesa kamili. Msomi huyo ambaye yuko kazini kwa miaka 30, mke wake ndiye Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Dk. Christine Ishengoma.

No comments: