na innocent munyuku
MAPEMA Juni mwaka huu, Klabu ya Yanga iliingia katika moja ya hatua ya maendeleo baada ya kupata ufadhili kutoka kwa Kampuni ya Gaming Management Tanzania Ltd inayomilikiwa na mfanyabiashara Yusuf Manji.
Ilikuwa hatua muhimu kwa Yanga kwani ni katika kipindi hicho, wanachama wa klabu hiyo walikuwa wakisigana na hivyo kuipa wakati mgumu timu ambayo kwa muda huo ilihitaji umoja ili ifanye vema katika Ligi Kuu Tanzania Bara na hivyo ndivyo ilivyokuwa, Yanga ni bingwa mwaka huu.
Mara baada ya kusaini mkataba huo, pande zilizokuwa zikitofautiana, Yanga Kampuni, Yanga Asili na Yanga Academia zikakubali pia kumaliza tofauti zao kwa maslahi ya Yanga na wanachama wengine.
Hakuna shaka kwamba ni Manji ndiye aliyeshinikiza kumalizwa kwa tofauti zilizokuwapo na akajitolea kuifadhili ziara ya wanachama wa Yanga chini ya Yusuf Mzimba katika mikoa mbalimbali kwa lengo la kufuta makundi na kambi zilizokuwa katika ugomvi.
Alipogusa klabu hiyo, jina la Manji licha ya kuwa lilishakuwa maarufu kabla, wapenzi wa klabu hiyo walimwongezea umaarufu kwa kumtukuza na kumwona kuwa mwokozi wa klabu hiyo.
Katika mahojiano maalumu na RAI mwishoni mwa wiki iliyopita, Manji anasema hakupenda kutukuzwa kwa kiasi kikubwa kama walivyofanya mashabiki na baadhi ya wanachama wa Yanga.
“Jina langu lilianza kupewa sifa kubwa kiasi kwamba sikupenda. Yanga walinichukulia kama mwanga na hali hii ilinitisha sana,” anasema Manji na kisha kuongeza:
“Yanga ilikuwapo tangu zamani na mimi lengo langu lilikuwa very simple, nalo ni vijana wawe nje na mambo yanayowaathiri kama vile ukimwi na dawa za kulevya.
“Nilianza kuwa na wazo hili tangu wakati wa maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa wabunge na rais mwaka jana. Kule Kigamboni nikawaahidi vijana kuwa nitawainua katika mambo mengi ikiwamo michezo,” anaeleza Manji ambaye katika uchaguzi huo alikuwa akiwania kupitishwa kuwania kiti cha ubunge.
“Kwa hiyo nikaona nini vijana wanapenda, nikagundua kuwa ni soka. Sasa nikasema kwa vile ni soka basi nitumie mwanya huo kuwatoa mitaani. Na njia mojawapo ni kuwainua wachezaji wa Yanga wawe bora ili vijana wengine waone fahari kucheza soka.
“Ulaya na sehemu nyingine duniani wana role models…mtoto anakua na kutamani maisha ya mtu fulani aliye juu katika jamii. Kwa hawa wa Yanga wakifanikiwa kuwa hapo ni wazi kuwa watakuwa walimu wazuri katika kuielimisha jamii.
“Beckham au Jay Z hawezi kutoka Ulaya kuja kutufundisha maadili hapa kwetu, tunatakiwa sisi wenyewe tufanye kazi hiyo.”
Anasema kuwa kutokana na kutambua hilo ndio maana akaona ni busara zaidi kuwajengea wachezaji mazingira mazuri kimapato. “Huwezi kuwa mchezaji bora wakati huna kitu…na idea yangu hapa ni kuwa na Ronaldo wetu.
“Kutokana na mawazo kama hayo ndio maana nasema na nataka nieleweke kuwa sikuingia Yanga kutafuta umaarufu bali kutimiza ahadi yangu kwa watoto niliyoitoa Kigamboni.
“Wapo walioifanya Yanga kuwa sehemu ya kupata umaarufu na pesa pia…lakini mimi si mmoja wao.”
Hata hivyo, Manji anasema kuwa pamoja na nia nzuri aliyo nayo, bado anahitaji ushirikiano wa hali ya juu na wadau wengine na kwamba lazima pesa anazotoa ziende kwa walengwa ambao ni wachezaji.
“Ninachoamini ni kuwa huwezi kuwa na timu bora kama huna wachezaji wazuri klabuni. Hawa wachezaji wakiwa na confidence uwanjani lazima wafanye vizuri na ndio maana ubingwa umekuja mapema.”
Kuhusu Yanga kuwa kioo cha jamii, Manji anaeleza kuwa mikakati inasukwa ili wachezaji siku zijazo waendeshe darasa la elimu kuhusu ukimwi au dawa za kulevya kwa vijana wenzao.
“Watapita (wachezaji) kila mahala kusema kwamba jamani hiki hakifai fuateni njia hii au fanyeni hivi hawa watakuwa sasa community hope.
“Lakini niwaambie kitu kingine kwamba Yanga has great future na ndio maana sikupenda kuona migongano ndani yake. Lazima tujadili tofauti zetu na sana sana tuwajali wachezaji kwa sababu hawa ndio kiini cha maendeleo.
“Ifike wakati mchezaji awe na heshima mtaani na si mtu wa kudharauliwa kwa sababu kama wataendelea hivi hakuna jema mbele yao na mbele ya Yanga pia.”
Lakini kuna jambo moja ambalo Manji katika mazungumzo yake hawezi kuliacha bila msisitizo nalo ni hisa kwa Yanga. Anasema lazima ununuzi wa hisa upewe kipaumbele kwani watu wengi au kampuni nyingi duniani zimefanikiwa kwa mtindo huo.
Kwamba ifike siku Yanga ijiendeshe kwa utajiri wake badala ya kumtegemea mtu mmoja au kampuni fulani.
“Leo hii tunawekeza na si jambo la busara kutegemea matunda leo, yafaa kuwa na subira lakini subira yenye matumaini ya maendeleo. Na lazima Yanga wajali umuhimu wa hisa.”
Katika mpango wa kuipa neema Yanga, Manji anasema kuwa utaratibu unaandaliwa ili kuanza kuuza fulana na kofia zenye majina ya wachezaji wa Yanga ili kutunisha mfuko wa klabu.
Anasema mapato ya mlangoni hayatoshi kuijenga klabu hiyo na kwamba mauzo ya fulana na mipango ifananayo na hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuijenga Yanga imara.
Monday, September 3, 2007
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment