Sunday, November 25, 2007

Tohara ya Ijumaa huanza Alhamisi

na innocent munyuku

KATIKA jamii nyingi za Kiafrika tohara ni mpango maalumu unaowalenga vijana wa kiume.

Mpango huo huwakusanya wahusika na kuwekwa jando ambako ni sehemu ya kufanyiwa tohara na kisha kupewa mafundisho kwa ajili ya maisha yao ya siku zijazo.

Hapa watafundwa juu ya ujasiri, uzalishaji mali na malezi kwa familia zao. Yaweza semwa kwamba jando ni pahala penye kutoa elimu kwa vijana.

Lakini kabla ya kuwekwa jando, huja maandalizi kwa ajili ya shughuli hiyo. Jando haliji kwa pupa kama kifanyavyo kimbunga. Mambo hupangwa yakanyooka.

Kutokana na umakini wa maandalizi hayo, ndio maana Waswahili wakaja na msemo kwamba tohara ya Ijumaa huanza Alhamisi. Kwamba kila jambo lafaa liwe na maandalizi badala ya papara.

Mzee wa Busati juma hili ameona anene juu ya hulka ya wadau wa soka nchini ambao kila uchao wamekuwa na ndoto ya kufika Kombe la Dunia lakini wanakwama kutokana na sababu mbalimbali.

Si mara moja au mbili washika kalamu na wenye uwezo wa kujenga hoja wameshasema juu ya vikwazo vilivyoko katika soka nchini.

Wameshahubiri juu ya nidhamu, programu endelevu, miradi na kubwa ni umuhimu wa kutambua kuwa soka nchini haiwezi kukua kama hakuna vitalu vya soka.

Mbaya zaidi ni kwamba wenye mamlaka katika uendeshaji wa mpira wa miguu nchini hawana jipya kwenye bongo zao.

Wamebaki kupiga porojo na kusahau kuwa pasipo vitalu vya soka mambo yatakwenda upogo.

Hao wamekaa kwenye viti wakisubiri kufika paradiso bila kuonja mauti. Wanahubiri na kuamini hadithi za Alfu Lela U Lela.

Wanaishi maisha ya kufikirika zaidi kuliko uhalisi wa mambo. Matokeo yake ni kwamba soka badala ya kupanda chati inageuka kuwa konokono kwenye sakafu iliyojaa chumvi. Vipaji vya soka vinapukutika.

Wamebakia kuamini ulozi kwenye viwanja vya soka na suala la maandalizi kwa miaka 50 ijayo hawanalo kwenye mipango yao. Wanawaza ya leo na si kesho.

Huko kwenye kusaka uchawi wameenea na idadi yao inaridhisha. Wamejaa tele kiasi kwamba hawaoni tena mwanga. Wamebaki gizani na wako radhi kuomba fedha kwa wafadhili eti kwa ajili ya kamati za ufundi.

Kamati ambazo wachezaji na viongozi waandamizi watalishwa madudu kama si kulala makaburi siku chache kabla ya mechi muhimu. Huo ndio mpira wetu!

Mzee wa Busati hasemi kwa ubaya bali kauli yake imetokana na kukerwa na haya magugu na mbigili kwenye soka.

Walau hivi karibuni wadau walipewa vidonge vya kule Bwagamoyo kwenye kile kilichoitwa semina elekezi ya wiki moja kwa klabu 14 za Ligi Kuu Bara.

Wakati wa kufunga semina hiyo, huku Mkurugenzi wa Maendeleo ya Soka wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Ashford Mamelodi akizitaka klabu kuachana na ndumba.

Alichosema Mamelodi siku hiyo ni kwamba makocha na viongozi wa soka nchini wanao wajibu wa kujifunza masuala ya ufundi na uongozi.

Mamelodi ambaye ni Mkurugenzi wa Maendeleo wa FIFA Kanda ya Afrika, aliwataka washiriki wa semina kuyafanyia kazi yote waliyojifunza kwa maslahi ya timu zao na soka kwa ujumla, huku wakiweka kando masuala ya imani za kishirikina au ndumba katika mpira wa miguu.

Akasema semina hiyo haitakuwa ya maana kama waliyojifunza hawatayafanyia kazi.

“…matarajio ni kubadilika kuanzia sasa, kuanzia masuala ya utawala hadi ufundi huku mambo ya kishirikina yakiwekwa kando,” alisema Mamelodi.

Hakuishia hapo, kiongozi huyo akaweka wazi kwamba klabu kongwe kama Simba na Yanga zafaa ziwe mfano wa kuigwa.

Kwamba timu hizo sharti zionyeshe dira ya mabadiliko na kuachana kabisa na mambo ya kishirikina dimbani. Huo ndio mtazamo wake ambao bila kigugumizi unaungwa mkono na Mwandika Busati.

Hii maana yake ni kwamba kama klabu za Ligi Kuu zitakuwa na mwelekeo sahihi hakuna shaka timu nyingine zitaiga ufundi huo.

Mpira wa miguu haupelekwi kwa ndumba bali ufundi na kupanga dira ya maendeleo. Huo ndio ukweli kuhusu soka.

Tanzania imejaa vijana wenye vipaji vya hali ya juu katika soka. Hata hivyo, vipaji hivyo vitaibuka kama viongozi wa soka watafuata utawala bora.

Vipaji hivyo vitavuma na kutamba kimataifa kama kutakuwa na mpango mzuri katika maandalizi ya mashindano na mgawanyo wa kazi na pia kuachana na migogoro.

Kuendelea na mtazamo wa kizamani ni ni kuifukia soka kaburini. Yafaa basi samaki akunjwe angali mbichi.

Mzee wa Busati anaamini kwamba kama maandalizi yatakuwa makini hakuna shaka kwamba Tanzania itatoa wachezaji wengi wazuri watakaotamba kimataifa.

Hilo linawezekana kama tutakubali na kutambua kuwa tohara ya Ijumaa huanza Alhamisi. Acheni papara kuweni na mipango ya maandalizi.
Wasalaam,

Sunday, November 18, 2007

Isikieni ndoto ya Msagasoli

na innocent munyuku

NI heri uchoke viungo vyote vya mwili kuliko uchovu wa ubongo. Hii ni hatari kubwa inayoweza kukufanya uonekane hamnazo kwenye kaya.

Bila shaka umeshawahi kukumbana na hali hiyo japo mara moja kila mwezi, iwe mwanzo wa mwezi au katikati yake. Ndo yalomkuta Mzee wa Busati juzi.

Mwandika Busati katoka kwenye mihangaiko yake huko mjini kati. Kasaka nyoka hadi soli za viatu zikaimba tungo za maombolezo.

Si mchezo mwanawane kusaga mguu kutoka Posta Mpya hadi Magomeni. Kisa? Kupunguza ukali wa bajeti ili mambo yasizidi kwenda upogo! Si ndo waambiwa mjini shule. Usione watu wana vitambi ukadhani maisha yao supa la hasha. Wengine wameshiba mihogo ilo chacha.

Mambo ya mjini ndivyo yalivyo. Usimwone jirani yako ananukia bia kila siku ukadhani anazo ngwenje za kutosha. Anachofanya ni kupitia kwa Mama Ubaya anaonja glasi zake tatu za machozi ya simba af baada ya hapo anapitia kwa Massawe anameza safari lager mbili kazi imekishwa.

Basi Mzee wa Busati baada ya kufika Magomeni na Sh 200 yake kibindoni akakwea daladala kuelekea maskani. Kutokana na uchovu wa kusaga mguu kutwa nzima mara baada ya kupata kigoda akautandika usingizi.

Yaliko maskani yake ni mbali na ukichanganya na foleni za Darisalama ni wazi kwamba alipata muda wa kuota ndoto pia na yaliyojiri kwenye ndoto ni haya yafuatayo.

Mzee wa Busati kaota eti yu katika kilele cha Mlima Kilimanjaro, kajiviringisha blanketi kuinusuru ngozi yake na baridi kali. Huko kileleni akaziona klabu za soka nchini zikiishi kwa upendo.

Akawaona wanachama wa Simba na Yanga wakipanga foleni ndefu kuwania hisa kwenye klabu zao baada ya kukubaliana kuwa sasa ziendeshwe kibiashara zaidi.

Akaiona pia Ashanti United, Moro United na Mtibwa Sugar zikifuata nyayo za Simba na Yanga. Hakuna tena uzandiki ndani ya klabu.

Wale wanachama waliokuwa wakitoleana maneno ya kejeli na matusi ya nguoni wakawa wameketi pamoja wakinywa kahawa na kupeana mawazo ya kuiinua soka nchini.

Ndoto ya Mzee wa Busati ikakatishwa na kelele za kijana muuza maji kwenye foleni. Hata hivyo, baada ya muda akaendelea kuuchapa usingizi.

Safari hii usingizi ukaja na ndoto mpya. Ndoto ikahamia kwenye filamu Tanzania. Mwandika Busati akawaona wasanii wakisaka elimu ya filamu kwa umakini.

Ile hali aliyozoea siku zote ya mtu mmoja kuamka tu asubuhi na kujiita prodyuza ikatoweka. Sasa hawa wakawa nguli wenye ustadi na kazi zao.

Akaziona filamu zilizopikwa zikapikika na si tena mpango wa kwenda dukani na kukuta video zilizotayarishwa kwa siku 28 eti nazo zikaitwa sinema kali.

Ndoto ikawa tamu kweli kweli manake hata wale wanamuziki ambao Mzee wa Busati alizoea kuwasikia wakiimba mapenzi tu na kusifia mavazi wakatoweka.

Kwenye ndoto yake akawasikia wakikemea ufisadi na wala rushwa waliovimba matumbo kwa sababu ya kula visivyo vyao.

Akasikia tungo zilizojaa uzalendo na kuwakemea wachache wanaouza nchi kwa njaa ya teni pasenti. Hao ambao hawajali kwamba milima ya Uluguru yafaa ilindwe kwa vizazi vijavyo.

Hao ambao wanajifanya hamnazo wasijue kuwa madini yetu ni mali ya kulijenga taifa kwa vitegemezi vyetu ambavyo baadhi yao havijui hata urithi wao.

Ndoto ikawa tamu zaidi manake akajikuta anazuru mitaa mbalimbali na kukutana na Watanzania wakijivunia utaifa wao. Wanateta Kiswahili kwa ufasaha.

Mzee wa Busati akawaona raia wengi wakiwania kuingia kwenye kumbi kuangalia ngoma na michezo ya asili. Wengi sasa wakawa wameyapa kisogo mambo ya Kimagharibi. Hakuna aliyejali tena ya kigeni.

Kina dada wakaachana na nywele za bandia. Sasa wengi wakawa wanalilia nywele zao za asili zenye kipilipili. Midomo ya wanawali hao ikapendeza kwa mdaha huku kucha ziking’aa kwa hina ya mwituni.

Honi ya lori kubwa ndiyo iliyomwamsha Mzee wa Busati usingizini akiwa ndani ya daladala. Anageuka kushoto anajikuta yu kituo kimoja kabla ya kufika anapoteremkia.

Anapangusa uso lakini moyo wake umejaa kero baada ya kubaini kuwa kumbe ilikuwa ndoto na dada aliyekuwa kulia kwake alikuwa na nywele bandia na rangi ya mdomo kutoka dukani.

Wimbo uliokuwa ukitoka kwenye spika za daladala ulikuwa ukimsifia jamaa aliyevaa mavazi ya kifahari kutoka ughaibuni.

Heri angesikia ngoma za Morris Nyunyusa au Mzee Mwinamila. Mzee wa Busati akanywea asipate raha ya ndoto yake.

Lakini je, hatuwezi kuishi kwa ndoto hiyo? Kweli Wabongo hawawezi kuendeleza utamaduni wao na kuacha kukumbatia yanayoonekana kwenye vioo vya luninga?

Hivi ni kweli klabu za soka haziwezi kujiendesha kibiashara na kuacha hii staili ya kushikiana bakora?

Mzee wa Busati amefikia ukomo akiamini kuwa kila mwenye ubongo uliotulia anao uwezo wa kuleta tafakuri na kuweka mwafaka kwenye bakuli.

Wasalaam,

Jihadharini na wafadhili wa siri katika siasa

Na Innocent Munyuku

HAKUNA jambo jema katika jamii kama uwazi na ukweli. Kwamba ili mambo yasiende upogo sharti mojawapo ni kuwa wazi na mkweli daima.

Kaya au jamii isiyo wazi mara zote itakuwa katika migogoro ya aina mbalimbali kwa sababu tu mambo mengi yamefichwa.

Kipato cha baba au mama kwa familia kikiwa siri basi hakuna shaka kwamba familia hiyo itakuwa kwenye mikwaruzo ya hapa na pale.

Wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa rais na wabunge mwaka 2005 kulikuwa na hoja kutoka kwa vyama vya Upinzani kwamba Chama Cha Mapinduzi kiliendesha kampeni zake kwa fedha ‘haramu’.
Watoa hoja hawakunyamaza bali wameendelea kulisema hilo hata baada ya uchaguzi kwamba sehemu kubwa ya fedha za kampeni kwa CCM hazikufahamika zimetoka wapi.

Wananchi wanaounga mkono upande wa Upinzani nao wanalijadili hilo vijiweni kila wanapopata muda wa kufanya hivyo.

Baada ya Rais wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Jakaya Kikwete kufunga Mkuu wa Nane wa chama hicho, mjini Dodoma siku chache zilizopita akiwa jijini Dar es Salaam alitoa kauli iliyonivuta kuandika waraka huu mfupi.

Rais Kikwete aliwahutubia wananchi waliomlaki Ofisi Ndogo ya CCM Lumumba jijini Dar es Salaam ambako pamoja na mambo mengine alisisitiza umuhimu wa chama kuwa na vitega uchumi.

Alichosema Rais Kikwete siku ile ni kwamba CCM ijipange kutafuta namna ya kuwa na vipato mbadala ili wakati wa kampeni kusiwe na minong’ono kuhusu vyanzo vya fedha.

Bila shaka kauli ya Rais imekuja baada ya kuzuka minong’ono kuhusu mapato ya CCM wakati wa kampeni kwenye uchaguzi uliopita.

Rais kanena umuhimu wa kuwa na vyanzo vya fedha vilivyo wazi kwa chama chake lakini kwa mtazamo wangu zumari alilopiga mkuu wa nchi ni vema likasikilizwa na vyama vingine pia.

Kwamba vyama vyote vya siasa nchini viwe wazi kuhusu mapato yake. Wawaeleze wananchi wanakopata fedha za kuzunguka nchi nzima kumwaga sera zao kwa ajili ya kujiongezea uhai wa chama na wanachama.

Leo hii ni jambo lisilohitaji mjadala mrefu kwani vyama vingi sasa vinaangalia namna ya kupata ushindi katika uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2010.

Kama inavyofahamika, kampeni zozote za uchaguzi kote duniani zinahitaji fedha za kutosha ili kuwafikia wapigakura. Hii maana yake ni kwamba vyama vinajipanga sasa kuangalia ni namna gani wanatunisha mifuko yao.

Lakini kwa bahati mbaya sana hapa kwetu hakuna utamaduni wa kuweka bayana juu ya vyanzo vya mapato kwa vyama vya siasa badala yake utasikia minong’ono kwamba mfanyabiashara fulani katoa kiasi fulani cha fedha.

Ingawa wapo wafanyabiashara wanaojitangaza wazi kwamba wametoa kiasi fulani cha fedha kwa chama fulani, bado ni haki ya wananchi kujua fedha nyingine zimetokana na nini.

Nasisitiza uwazi wa vyanzo vya fedha kutokana na ukweli kwamba yawezekana ikaja siku, fedha za kampeni zikatokana na mauzo ya dawa za kulevya au njia nyingine haramu hatarishi kwa taifa lililo huru.

Tuelezwe pasipo kificho kwamba mabilioni haya yametokana na michango ya aina hii au msaada kutoka taasisi fulani iwe ya ndani ya nje ya nchi.

Kama ni fedha za wafadhili pia tuelezwe ni wa aina gani na zimetolewa kwa masharti gani.

Kukaa kimya hakuna maana nyingine zaidi ya kuendelea kuzua minong’ono ambayo ingeweza kufutwa kama kila kitu kingewekwa hadharani.

Nalisema hili kwa sababu mwaka 2010 si mbali kutoka hivi sasa na bila shaka baadhi ya vyama vya siasa vimeshaanza kukusanya fedha kwa ajili ya uchaguzi ujao.

Hivyo basi, wakati ukifika ni busara kuwaeleza wananchi nani kafanya kipi kufanikisha mizunguko ya kampeni.

Vinginevyo ipo siku tutashuhudia wafadhili wa siri wakidai kulipwa fadhila kwa mtindo wa kuliangamiza taifa. Tusifikishane huko.

Monday, November 12, 2007

Mkiitwa majinuni msirushe ngumi

na innocent munyuku

IKITOKEA binadamu akatoa maneno ya vichekesho na yasiyo na maana basi huyo ataitwa majinuni. Huyu hupachikwa kofia hiyo kwa sababu hana akili sawa sawa.

Pahala pengine mtu wa aina hiyo hutajwa kuwa ni punguani, mwendawazimu, kichaa ama wakati mwingine huitwa bahau.

Yawezekana mtu wa aina hiyo asifikie hatua ya kuvua nguo hadharani na kusomba kila akionacho lakini ukweli ni kwamba wapo binadamu ambao katika utendaji wao wa kazi hawana tofauti na vichaa wanaozagaa mitaani.

Ukiona dereva anayevunja sheria za usalama barabarani kwa kupenda mwendo kasi katika eneo lililokatazwa basi huyo ni punguani.

Hali kadhalika kwa muuguzi na daktari kutenda yasiyotarajiwa katika fani yao hapo watakuwa wamejihalalishia kuitwa vichaa au wendawazimu.

Mzee wa Busati leo wiki hii ameona ni vema kuwekana sawa katika majukumu ya kila siku kwenye klabu za soka.

Usiposikia moto wawaka Yanga basi ni Simba au kwenye vyama vya soka ndani ya Tanzania. Huko ni vurugu mtindo mmoja.

Huko utakutana na mahuluti kwa maana ya mchanganyiko wa watu wenye mawazo tofauti. Huyu anawaza begi mwingine anafikiria sanduku.

Kwa maana hiyo hata wanapoketi kwenye mikutano na kuleta mjadala, hakuna linalokwenda sawia. Hayaendi sawa kwa sababu kila mmoja la lwake.

Kuna msemo maarufu kwenye klabu hizo za soka. Kwamba uongozi umepinduliwa. Hii ni staili ya miaka mingi nchini. Kundi fulani la kihuni linajikusanya na kutangaza maasi.

Hilo si kwa Simba pekee bali hata Yanga. Kwa maneno mengine jambo hilo lipo kwenye ndimi za wanachama wa klabu hizo kama ilivyo sala ya ‘Baba Yetu’ kwa Wakristo.

Ni heri kwao wanaojiita wanamapinduzi wakaja na fikra pevu za kujenga klabu na soka kwa ujumla. Wangeleta mageuzi chanya na si hasi kama wafanyavyo sasa.

Kwa mtazamo wa Mzee wa Busati kinachofanywa kwenye klabu hizi ni uhuni usiokuwa na mfanowe. Ubabaishaji uliojaa simulizi za lege lege.

Mwenye Busati pengine aulize, kwa mfano hili fukuto la Simba kati ya kina Rubeya na Dalali nani ananufaika nalo? Kelele kibao na ghasia ambazo zingeweza kuzuilika.

Leo twaimba wimbo wa kuijenga Tanzania katika medani ya soka. Miezi michache nyuma sifa ziliwaelemea wachezaji wa timu ya taifa waliokuwa wakisaka tiketi ya kwenda fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika nchini Ghana.

Bendera na fulana zikachapishwa kwa wingi, wenye bahati zao msimu huo ukawa wa mavuno. Wakajaza pochi zao kwa ngwenje kwa kuuza sura za kina Mapunda na Henry Joseph.

Ingawa safari ya Ghana imeota mbaya ukweli wa mambo ni kwamba mshikamano ule wa mashabiki wa soka haukuwa na maana nyingine zaidi ya mapenzi kwa timu yao ya taifa.

Wabongo wamezoea kuzililia Simba na Yanga lakini siku ile Msumbiji ilipomaliza ndoto ya Stars kwenda Ghana, waliungana kwa kilio na majonzi. Huo ni mshikamano wa dhati.

Taswira hapo ni kwamba walio wengi wanapenda soka lakini wanakwamishwa na utawala hasa katika ngazi za klabu. Huko kuna mbigili na magugu sugu.

Anachosema Mzee wa Busati ni kwamba wahuni waliojaa kwenye klabu za soka nchini ndio wanaosababisha kukwama kwa uundaji wa timu ya taifa makini.

Hivi mwatarajia kuwe na timu ya taifa yenye ubora wakati huko chini ni vurugu tupu? Nani kawafunda hayo?

Uhuni na uzandiki unaoendelea katika soka hivi sasa hauna lolote la maana zaidi ya kuua mwelekeo mwema wa soka.

Soga na porojo zinazoendelea katika klabu za soka hazina budi kukomeshwa kwa maslahi ya taifa. Vinginevyo tukubali kuendelea kuwashabikia wenzetu wa ng’ambo.

Endeleeni kuvuruga ili mbaki kuvaa fulana za wachezaji wa ughaibuni huku wa kwenu wakikaa vijiweni kusubiri mia mbili ya kahawa.

Lakini Mzee wa Busati kabla hajafikia ukingoni pengine aweke mambo hadharani kwamba kwenu nyie mnaovuruga mambo ya soka msije kurusha ngumi siku mtakapoitwa majinuni.

Msihamaki wala kushika panga kwani hiyo ni halali kwenu. Kuitwa wehu ni zawadi mwafaka kwenu na wahuni wenzenu wanaowarubuni kuharibu mambo.

Mwandika Busati katoa mwanga. Wapo wengine wenye uwezo wa kuasa ni heri wakafanya hayo ili taifa lisiwe la mabahau.

Wasalaam,

Wednesday, November 7, 2007

Ranking Boy: Reggae ilete mijadala yenye suluhu

na innocent munyuku

KAMA ningetakiwa kuwataja wanamuziki wa reggae wenye dira njema ya maelekeo nchini basi nisingesita kumweka Ranking Boy kundini.

Hivi karibuni mwanamuziki huyo amefanya mahojiano na Mtanzania na kuweka wazi mikakati yake na vikwazo katika muziki huo nchini.

Ranking Boy ambaye si mzungumzaji lakini mahiri jukwaani ashikapo maikrofoni upole na ‘ububu’ wake hauonekani. Anatema cheche za ajabu akitoa elimu na burudani.

Ana mambo mengi anayoyaandaa mojawapo ni kuipua albamu yake mpya mapema mwezi ujao. Albamu hiyo ameipachika jina la More Than Dread.

“Natarajia albamu yangu ya More Than Dread itakuwa sokoni mapema Desemba na itatoka pamoja na video yake,” anaeleza Ranking Boy.

Mwanamuziki huyo mbali na kuimba reggae anamudu pia raga na midundo dance hall huku akiwa na uwezo wa kutumia ala mbalimbali.

Alianza kujikita katika fani ya muziki mwaka 1998 na baada ya siku chache akahamishia makazi yake nchini Kenya na Uganda akifanya kazi zake za muziki kwa miaka minne nje ya Tanzania.

Ni katika kipindi hicho, Ranking Boy alifanikiwa kufyatua single nne ambazo ni Medicine, Matatizo, Fiesta na Ghetto.

“Nyimbo zangu kwa kweli zinajieleza kwa mfano wimbo wa Matatizo nimesema ukweli juu ya hali halisi ya maisha ya kila siku,” anasema na kisha kuongeza:

“Kila kukicha nchi inaendelea kuwa masikini na watu kwa hakika wanataabika…kwa hiyo nimejaribu kuelezea hali hiyo katika wimbo wangu huo.”


Anasema baada ya kuishi nje ya Tanzania kwa takribani miaka minne aliamua kurejea nchini kuendelea na shughuli zake za muziki wa reggae.

“Mwaka jana nikatua nchini kwa lengo la kuendeleza muziki wa reggae. Nikaja na wimbo wa Fire Ban Dem Head. Nashukuru kwamba single hii ilifanya vizuri na redio nyingi wameendelea kuupiga.

“Kufanya vizuri kwa wimbo huo kukanipa nguvu sana na ndio maana si rahisi kusema kuwa naweza kukata tamaa,” anasema mwanamuziki huyo ambaye tayari ana albamu nyingine ya Dad Fred.

Ranking Boy kwa sasa anaandaa kuzindua mradi maalumu wa muziki wa reggae aliouita Reggae Search utakaodumu kwa mwaka mmoja.

“Lengo la mradi huu ni kuwakusanya wasanii wachanga wa muziki wa reggae na kuwapa dira mpya.

“Muziki wa reggae lazima tukubali pia unahitaji fikra mpya. Hatuwezi kuishi kama walivyoishi wanamuziki wa kale mambo yamebadilika,” anasema na kuongeza:

“Lakini hii haina maana kwamba tunakwepa misingi ya muziki wa reggae hapana. Ninachosema ni kwamba tuwe tayari kwa mabadiliko.”

Anasema anaamini kuwa kuwa na vijana wadogo katika reggae kutawezesha muziki huo kuwa na uhai hasa katika Afrika.

“Mpango wa kuwasaka vijana umeshaanza na hii naweza kusema kuwa ni project ya Afrika Mashariki nzima.

“Kwanza tutawafundisha hao wachanga na baadaye kuwapa muda wa kutunga nyimbo na hapo tutaangalia wimbo gani bora. Lengo hapa ni kuleta ushindani,” anasema.

Anaeleza kuwa anafarijika kuona kuwa wadau wake kutoka Uganda na Kenya wanatoa ushirikiano mzuri na hivyo anaamini kuwa mradi huo wa reggae utazaa matunda mema.

“Ushirikiano unatia moyo kwa kiasi kikubwa, watu wana mwamko sana. Naweza kusema kuwa sasa reggae inakwenda katika neema zaidi kuliko miaka ya nyuma.”

Lakini anasisitiza kuwa kuna haja ya wanamuziki wa reggae kwenda mbele na kuacha imani kwamba lazima kuiga kila jambo la waliopita.

“Kila kizazi kina mambo yake. Ya kale ni kama mwongozo kwamba wenzetu walifanya nini na sisi kazi yetu ni kuboresha.

“Nitatoa mfano kwamba enzi za kina Kalikawe si za sasa na kama mimi sasa nakuja na mtindo wa Bongo Jamaica.

“Bongo Jamaica ni mtindo mpya ambao ni mchanganyiko wa vionjo kutoka Jamaica na ukanda wa Afrika Mashariki. Nami muda wangu ukimalizika watakuja wengine na vionjo vyao,” anasema Ranking Boy.

Hata hivyo, bado anasisitiza kuwa kazi kubwa ya muziki wa reggae ni kuleta mapinduzi ya fikra.

“Huu si muziki wa porojo, muziki wa reggae lazima ulenge mabadiliko katika jamii na si malumbano au hoja ambazo hazina kichwa wala miguu.

“Reggae ilete mijadala yenye ufumbuzi na si kujadili mambo ambayo hayana suluhisho,” anasema Ranking Boy.

Pamoja na hilo, Ranking Boy anasema kuwa katika muziki wa reggae nchini kuna kikwazo ambacho hakina budi kuondolewa.

Anasema tatizo kubwa miongoni mwa wanamuziki hao ni kukosa ushirikiano wa dhati.

“Inashangaza sana na binafsi jambo hili linanikera kwamba hatuna ushirikiano wa kweli. Huo ni uwazi kwamba hatuna umoja.

“Kila mmoja yuko kivyake na hii maana yake ni kwamba mipango mingi itavurugika na tutabaki kulalama.”

Pamoja na yote hayo, msanii huyo ana faraja kuona kuwa muziki wa reggae kwa kiasi kikubwa unakubalika nchini.

“Zamani ilionekana kama kuimba reggae ni kuhamasisha uvutaji bangi lakini sasa mambo yamegeuka hata watu wazima wanapenda reggae,” anaeleza Ranking Boy.

Monday, November 5, 2007

Wasanii mtapakwa tope hadi lini?

na innocent munyuku

SIKU zinasonga mbele na kinachohesabiwa sasa ni namna ya kuhitimisha mwaka kwa nguvu za Mola.

Hakuna mwenye uhakika wa moja kwa moja kama ataiona Januari Mosi ya mwaka 2008. Badala yake wengi wanaendelea kupiga dua, waendelee ndani ya dimba wasikalishwe benchi.

Mwandika Busati naye yu katika sala akiomba kwa nguvu zote ili auone mwaka mpya kwani kapanga mengi ya neema kwa mwaka ujao.

Tukiachana na dua za mwaka mpya, Mzee wa Busati juma hili anakuja na dukuduku lake ambalo kadri siku zinavyoyoma ndivyo anavyoumia kwenye mtima.

Limekuwa jambo la mazoea sasa kwa mtu fisadi, mshenzi au tapeli kuitwa ‘msanii’. Hilo ndilo jina la ubatizo kwa watu wa jamii hiyo.

Kwamba watu waongo wenye upande hasi katika kaya zetu huitwa ‘wasanii’. Hili jambo kwa hakika linakera nafsi hasa ya Mzee wa Busati.

Linakera kwa sababu hakuna njia nyepesi ya kuliezea hili zaidi ya ukweli kwamba wasanii nchini wanadhalilishwa na kupakwa matope.

Ajuavyo Mzee wa Busati ni kwamba tafsiri rahisi ya msanii ni mtu mwenye ustadi wa kuchora, kuchonga, au kutia nakshi.

Lakini pia pahala pengine, msanii hutajwa kuwa ni mtu mwenye ufundi wa kutunga na kutoa mawazo yake kama vile kwa kutoa shairi, hadithi au tamthiliya.

Leo hii sifa hizo nzuri zimetoweka na wajuzi wameamua kuwapaka matope wasanii kwa kuwahusisha na yasiyofaa.

Tapeli na wasio makini katika jamii huitwa wasanii. Wahuni na wababaishaji leo hii wamepewa jina la usanii. Hii maana yake nini?

Huku ni kudhalilishwa, wasanii wamevuliwa nguo na hakuna anayeonekana kujali. Wamepakwa matope nao kwa unyonge wao ni kama waliokubali hali hiyo.

Hivi kwanini basi waongo na matapeli wasiitwe wahandisi, madaktari, wauguzi, walimu au marubani. Iweje msanii ndiye apakwe tope? Huku ni kudhalilishana.

Mzee wa Busati analia na hili kutokana na ukweli kwamba kuna upotoshaji wa makusudi katika hadhi ya wasanii nchini na pengine duniani kote.

Twawafunda nini vijana wetu wanaochipukia? Tunawalea kwa mtindo gani? Makuzi yao twayapotosha kwani kuna hatari jinsi wanavyokua wakakosa hamu ya kujiingiza katika sanaa.

Hawatakubali kwa sababu tayari wameshanasa vichwani mwao kwamba wasanii ni watu wa hovyo wasio na mwelekeo mwema katika jamii.

Watakimbia kwa vile wamefundishwa kwamba msanii si lolote. Watabaki kufifisha vipaji vyao na hii maana yake ni kwamba jamii itakosa wabunifu na waburudishaji.

Lakini pengine kuna haja ya wasanii kutoa tamko la kulaani hali hii ambayo sasa imezoeleka ndani ya kaya zetu. Amkeni mseme kwamba wasiendelee kugusa mboni za macho yenu.

Msikae kimya manake kimya chenu kitachukuliwa kuwa tayari mmeridhia kuchafuliwa kwa kiwango cha hali ya juu. Itasemwa kwamba ndivyo mlivyo kwani hakuna pahala mmewahi kukemea jambo hilo.

Vinginevyo Mzee wa Busati anaelekea ukingoni akiangalia namna Wanamsimbazi wanavyoendelea kuvutana kwa kile kinachosemwa kwamba kusafisha uongozi.

Simba wa Yuda na Mwenyekiti wake na wengine wanne wamepigwa chini kwa madai ya ‘kutafuna’ fedha za chama na ulegevu wa timu katika Ligi Kuu Tanzania Bara.

Hao wamesomewa tuhuma 10 na hivyo wanachama 271 kuridhia kupigwa chini kwa Simba wa Yuda na bosi wake. Wamesimamishwa lakini je, hiyo ni suluhu ya mambo ndani ya Simba?

Hofu ya Mzee wa Busati ni kwamba isije ikaja kesi ambayo itaendelea kuvuruga klabu hiyo yenye mashabiki tele ndani ya Tanzania.

Msije mkajikuta mmekwamba sehemu kwenye mto wenye mamba wenye njaa kwani huko hakuna salama hata kidogo. Huo utakuwa mwisho wenu wa kila kitu.

Mnachokifanya sasa ni kuanza kutafunana. Mtawatafuna sita baadaye saba hadi 10 mwishowe mtajitafuna na kumalizana na huo utakuwa mwisho wenu.

Kwamba moto huu uliowashwa Msimbazi usije unguza kila kitu na kuyaacha mahame.

Wasalaam,

Friday, November 2, 2007

Yarab epusha hasira zao zisivuke mpaka

Na Innocent Munyuku

KWA zaidi ya miezi 12 sasa, Watanzania wengi wamekuwa wakitupa lawama kwa Serikali kwamba imeshindwa kutekeleza ahadi zake kwa maslahi ya umma.

Wanacholalamikia ni hali duni ya maisha waliyonayo. Wengi wao hawana ajira na hivyo kuwawia vigumu kupata mahitaji yao ya kila siku kama inavyostahili.

Wanacholilia ni maisha bora na ajira zitakazowawezesha kuwa na vipato vya uhakika vya kutoshelezesha mahitaji ya msingi katika ustawi wa jamii.

Vilio ni kila mahala, kwani ukweli wa mambo ni kwamba, ukali wa maisha ungali ukiendelea kutokana na hali halisi ya upandaji bei katika bidhaa mbalimbali.

Sehemu kubwa ya Tanzania kinachoimbwa na wananchi ni ugumu wa maisha. Wengi sasa hudiriki kusema ya kuwa, maisha ya leo nafuu ya jana, wakimaanisha kwamba kila uchao mambo yamekuwa ya kukatisha tamaa.

Na ndio maana, hivi karibuni baadhi ya mawaziri walipozuru mikoani kuelezea ‘uzuri’ wa bajeti ya mwaka huu wa fedha 2007/08 walizomewa na wananchi.

Binafsi, habari kwamba baadhi ya mawaziri walizomewa huko mikoani na hivyo kuwa shubiri kwao ilinishangaza kidogo, lakini pia ikanifunza jambo moja kwamba sasa watu wamechoka!

Kwamba kama imefikia mahala wananchi badala ya kusikiliza hotuba za mawaziri wanawatolea maneno ya kejeli na kuwazomea, hili jambo si la kupuuzia au kuliacha hivi hivi.

Sauti zile zina maana yake na kama sitakwenda mbali na ukweli, ni kwamba watu sasa wamekata tamaa na ndio maana mazungumzo katika kila kona ya nchi ni mjadala kuhusu maisha bora.

Mwaka 2005, bei ya mkate wa kawaida kabisa ilikuwa kati ya Sh 200 hadi Sh 300. Leo hii mkate huo unaliwa kwa Sh 500 hadi Sh 700. Si mkate pekee bali karibu kila bidhaa imepanda bei.

Ndicho wanacholalamikia raia wa nchi hii kwamba sasa mambo ni magumu na kwa hakika hawaoni pa kutokea labda kwa nguvu za Muumba.

Sasa hivi kuna hili wimbi la kile kinachoitwa ‘orodha ya mafisadi’. Wananchi wengi wanaendelea na mijadala kila wapatapo nafasi ya kusema juu ya jambo hilo. Wanajadili hoja hizo za wapinzani na kwa vile Serikali imeamua kutulia, nao wanajawa na maswali tele kwenye vichwa vyao.

Wanasema juu ya mfumo mzima wa mikataba ya wawekezaji wa madini nchini. Na ndio maana huko North Mara mwezi uliopita, wananchi waliishambulia kwa jiwe helikopta ya wawekezaji.

Katika shambulizi hilo, kioo cha helikopta hiyo kilitobolewa na rubani wake kuumizwa jicho. Hii maana yake ni kwamba, kama wananchi hao wangekuwa na silaha ya kisasa wangeleta madhara makubwa.

Hawa wana hasira na wawekezaji ambao wanaendelea kuchimba madini yetu na kutuachia mahandaki. Mwananchi wa kawaida haelewi manufaa katika miradi hiyo ya madini, anachojua ni kwamba kuna hitilafu.

Anaamini kuna hitilafu, kwa sababu bado maisha yake yameendelea kuwa ya dhiki. Anachoamini ndicho hicho kwamba nchi inaliwa na wachache.

Hapa kuna ulazima wa kuyaweka haya mambo bayana. Kwamba hakuna maana njema kuendelea kushabikia misaada ya wawekezaji hao kama hakutakuwa na uwiano unaoeleweka juu ya wanachokipata na wanachokiacha kwa wananchi.

Hatuwezi kuchekelea miundombinu kwenye migodi hiyo kwa sababu ni wazi kwamba imewekwa kwa ajili ya kurahisisha utendaji wao wa kila siku.

Pengine nirejee mfano wa kombeo lililotumika kurusha jiwe lililoharibu kioo cha helikopta North Mara. Aliyerusha ni wazi alikuwa amejaa hasira akiamini kwamba nchi yake inafilisiwa. Akashindwa kujizuia akafanya alichofanya.

Leo hii wametumia kombeo, kesho watakamata chupa na jambia mkono mwingine. Wakiona mambo bado hayaendi, si ajabu wakaamua kuingia mitaani wakiwa na kila kinachofaa kubebeka.

Hili halitashangaza, kwani tayari wameshaanza kuvamia vituo vya polisi na wala hakuna mwenye hofu ya kutwangwa risasi za moto. Wananchi wanaonyesha wazi hasira zao kwa dola.

Hawatajali, kwa sababu maisha yao tayari yamekwenda upogo na hawana tena imani ya kufika nchi ya ahadi yenye maziwa na asali ya mwitu. Wataona heri wafe wakidai wanachoamini kuwa ni haki yao.

Wamechoka kwa sababu wanaona kila kitu hakiendi katika mstari unaofaa. Misaada ya nchi za nje inatumikaje? Ndivyo wanavyojiuliza.

Kuna watu leo hii wana vitambi vya ukimwi, magorofa ya ukimwi na hata magari ya kifahari ya ukimwi. Hawa wametafuna fedha za wahisani zilizolenga kuwasaidia waathirika wa ukimwi. Wakageuka wajanja wakaziweka kwenye mifuko yao.

Wajanja hawapo kwenye miradi ya ukimwi pekee, wapo kila mahala wakiwa mahiri wa kuandika ‘proposals’ za kuombea fedha za wafadhili katika miradi mbalimbali. Mingi kati ya hiyo ni yao binafsi wakila na kusaza pasipo woga.

Leo hii, hawa ndio wafalme wanaotembea kwa kujiamini wakikanyaga ardhi ya Tanzania kama ya kwao pekee. Hawa ni wateule ambao wamesimama sawia na si rahisi wakapigwa mwereka.

Lakini, hoja ya msingi hapa ni kwamba dhana ya uwiano wa maisha kwa raia wa taifa hili lazima ijadiliwe kwa mapana kwani uwezo wa kuwawezesha wananchi upo kutokana na ukweli kwamba bado tunazo rasilimali za kutosha.

Nionavyo mimi ni kwamba, kuna haja basi kukawa na jukwaa huru ambalo wananchi wa kawaida watapata mwanya wa kuwaeleza watawala wao kero na dhiki zao.

Watawala wasikae kimya au kupangua hoja kwa msimamo wa kisiasa kwani ni ukweli usiopingika kuwa maisha sasa ni magumu na yanaendelea kuwa magumu.

Wananchi wanahoji mengi na wana shaka kama wasaidizi wakuu wa watawala wanayafikisha kama yalivyo au wanaondoa ukakasi kabla ya Mkuu wa Kaya hajasoma ripoti zao.

Sidhani kama anaelezwa kero kwenye vituo vya polisi, mahakama, hospitalini au katika ofisi nyingine za Serikali ambako usumbufu wa kupewa huduma umerejea kama miaka ya nyuma.

Kama haya yataendelea, basi ni wazi kuwa wananchi watachoka na kitakachofuata ni vigumu kusema kwamba kitakuwa cha heri. Basi na tumwombe Muumba tusiione siku hiyo.

0754 471 920