na innocent munyuku
YAMETIMIA! Hadithi imekuwa ile ile kwa Tanzania kuangukia pua kwenye mashindano ya urembo ya dunia.
Binti aliyelalamikiwa hadi koo kuwaka moto, Richa Adhia aliyeiwakilisha Tanzania katika Miss World amevurunda na wala hakupata nafasi ya kufurukuta.
Kilichosemwa na mrembo huyo ambaye rangi yake ilimweka mbali na mashabiki wengi wa urembo akasema kuwa Kamati ya Miss Tanzania imechangia yeye kuboronga.
Kimwana huyo akaweka wazi kwamba Kamati ya Miss Tanzania ilishindwa kuwahisha DVD yenye shughuli alizozifanya baada ya kuwa mrembo wa Tanzania katika Kamati ya Miss World.
Anacholalama Richa ni kwamba kama DVD yake ingewahi angekuwa na nafasi ya kushinda katika kipengele cha Urembo wa Malengo.
Hii ni bahati mbaya kwa mlimbwende huyo na wadau wa urembo nchini. Lakini yaweza semwa pia kuwa bado kuna kikwazo katika mchakato mzima wa kumsaka Miss Tanzania.
Mzee wa Busati alikuwa mmoja wa walionyesha shaka juu ya uwezo wa kimwana huyo katika uwakilishi wake katika mashindano hayo ya dunia.
Alichosema Mwandika Busati wakati huo ni kwamba ushindi wake ulijaa shaka na hata ndimi za mashabiki zimeendelea kuwa hivyo. Wengine wakasema pia kuwa kwani kulikuwa na ulazima gani wa kumvisha taji na kimwana huyo mwenye damu ya Kihindi?
Wanaojiita wanaharakati na watetezi wa haki za binadamu wakasema kuwa huo ni ubaguzi wa rangi. Lakini hoja ikabaki ile ile kwamba je, mrembo huyo anaujua vema utamaduni wa Kitanzania?
Pengine hoja hizo hazina nguvu tena kwani mambo yamekwenda na yamesikika sasa kilichobaki ni wenye mamlaka na urembo wajipange upya.
Lakini wakati wanajipanga upya Mzee wa Busati anawaza jambo moja ambalo laweza kuijengea heshima na Tanzania kwa ujumla wake.
Kwanini basi tusisitize kuwapo kwa Miss Bantu? Mashindano ambayo kwa hakika yanalenga moja kwa moja asili ya kina dada wengi hapa Bongo.
Kuwa Miss Bantu si jambo gumu kwa sababu kwa baadhi ya vigezo ambavyo Mwandika Busati anavielewa ni kwamba binti hahitaji kuwa mwembamba ili kupata sifa ya kupanda jukwaani.
Hiyo ndiyo burudani ya Miss Bantu. Kimwana na ‘minyama’ yake anakuwa huru kupanda jukwaani kusaka ushindi mbele ya majaji.
Hii maana yake ni kwamba mabinti washiriki hawabanwi kula na kunyaza miili yao. Inasemwa pia kuwa hata lugha si kikwazo, unanena Kiswahili utakavyo na wala hakuna haja ya kwenda inglishi kozi.
Mtazamo wa Mzee wa Busati ni kwamba kama mashindano ya Miss Bantu yatawekewa mkazo basi nasi siku moja tutaungana na Wakongo, Warundi, Waganda na Wakenya na kuanzisha mashindano ya kanda.
Wakifikia hatua hiyo ni wazi kuwa Afrika itakuwa na kitu chake manake matarajio ni kwamba yatapanuka hadi kwingineko.
Ndoto ya Mzee wa Busati ni kwamba ifike siku hata Wazungu na Wahindi vibonge nao waje washiriki mashindano hayo. Hata kama wao si Wabantu waruhusiwe kwa sifa yao ya ubonge.
Kwanini yatuwia vigumu kuamini mambo mema ya kwetu? Kwani lazima tufuate kila kitu kilichoanzishwa Ulaya? Bila shaka hakuna haja hiyo. Yawezekana mengine yakaanzia Afrika na kuwashangaza walioko nje ya Afrika.
Huo ni mtazamo tu na si lazima wote mkubaliane na Mwandika Busati leteni hoja zenu kwa mjadala na lengo liwe kufikia mwafaka.
Huenda ikasemwa kuwa Mzee wa Busati ni mwepesi wa kukata tamaa la hasha! Mwelekeo wetu katika mashindano hayo ya Wazungu si mwema na siasa za Miss World katu hatuziwezi.
Si mmesikia wiki iliyopita warembo kutoka Afrika walivyokuwa wakilalama? Walikuwa wakilalamikia ubaguzi. Walichosema wala si uzushi ni ukweli na wazi wa mambo.
Basi himizeni mashindano yenye kufanana na utamaduni wetu. Waacheni warembo wetu wa Kiafrika wawe na pahala pa kujitanua.
Msiwashindishe njaa eti ili waonekane warembo wenye sifa za kupanda jukwaani kuwania taji la Miss World. Waacheni wale matoke na maharagwe.
Vinginevyo kung’ang’ania hayo ya ughaibuni ni kuzidi kujaza nafasi na ghasia kwenye ardhi ya Wadanganyika.
Huu ndio ukomo wa Mwandika Busati kwa juma hili. Mwendo mdundo kwa kasi ya ajabu manake ujio wa Masiha unayumbisha fikra.
Ngwenje zinasakwa kwa kila mtindo, kihalali na kiharamu ili mradi mifuko yao ijazwe fedhwa kwa ajili ya Noeli na mwaka mpya.
Wasalaam,
Tuesday, December 4, 2007
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment