Sunday, May 4, 2008

Hata walimbwende wanaulea ufisadi

Na Innocent Munyuku

USIOMBE kuzimika ghafla kwenye steji. Ni kama vile kifo cha penzi kinavyokuwa. Ni shubiri kwa kwenda mbele. Msosi hauliki mwanawane.

Mzee wa Busati kaleta kero, alitokomea gizani na mbaya zaidi ni kwamba hakuwa na uungwana wa kutoa neno la kwaheri. Yalomkuta ni siri yake ila ukweli ni kwamba kishapewa notisi yenye maelekezo machungu.

Watoa notisi ambao ni wadau wake wamemweleza wazi kwamba kama akirudia kutenda aliyoyatenda yaani kuzimika pasipo taarifa basi asubiri kumwagiwa upupu. Hakika ni adhabu kubwa.

Kwa hakika Mzee wa Busati anastahili adhabu kwani huo kwa kweli ni uhuni kama afanyavyo Mzee wa Kutibua ambaye yeye anaweza kuamua kulala popote hata kama kaunta kilevi kikimkolea. Ipo siku atajuta!

Tuachane na hayo, bila shaka wadau wameelewa somo kwani kuzimika kwa Mwandika Busati hakukuwa katika utani bali alikuwa akiwajibika katika masuala mengine ya kitaifa kule Idodomya kwenye jengo linalopitisha sheria. Mhh samahani wanasema ni jengo la watunga sheria.

Huko Mzee wa Busati kawa shuhuda wa mambo mengi, mema na mabaya. Ila alilofurahia Mwandika Busati ni kuona kuwa kumbe kuna majimbo ya uchaguzi ambayo ni kama hayana wabunge.

Kwamba yaliyo mengi yana wawakilishi bubu, hawasemi hawa, ndimi zao zimenasa wasipate kutoa sauti hata ya kuuliza suala mojawapo la jimboni kwake.

Mbaya zaidi ni kwamba kati ya wabunge hao ‘mabubu’ wanatoka sehemu ambako umasikini umekithiri. Cha ajabu ni kuwa wabunge waliotoka kwenye neema ndio wanaopaza sauti kudai tija kwa wapigakura wao. Hakika wonders will never cease.

Anyway hebu sasa turejee kwenye porojo zetu za kispoti na burudani. Hayo ya siasa hayafai manake unaweza ukijikuta unabadilishwa jina muda si mrefu. Wenye majimbo wasije wakatukimbiza mjini.

Pamoja na Mwandika Busati kuwa kimya kwa zaidi ya majuma mawili, ukweli wa mambo ni kwamba amekuwa karibu na kila jambo linalopita mjini.

Mojawapo ni haya maandalizi ya kusaka vimwana katika hatua za vitongoji na hatimaye kuingia kwa shindano la taifa la kigoli wa Tanzania.

Mawakala wa vitongoji wameshaanza kuingia mtaani kusaka fedha na mambo mengine ya kukamilisha mashindano. Mabingwa wa kuandika propozo za kuomba udhamini huu ni wakati wao wa kujidai.

Mabingwa wa kuongeza cha juu nao ni wakati wao wa kujaza matumbo kwani raha ya udhamini kwao nafasi zao ni kujaza fedha mfukoni ili mambo yawaendee sawia.

Hata hivyo, kwa mtazamo wa Mwandika Busati ni kwamba kuna ulazima wa kuweka mikakati ya makusudi katika maandalizi hayo hasa kutokana na historia ya mashindano hayo nchini.

Kila mwaka kero huwa ni zile zile; kashfa za ngono, upendeleo usio wa lazima katika kuwapata washindi na wakati mwingine utapeli kwa baadhi ya mawakala.

Ndimi za baadhi ya mawakala hujaa neema wanapotangaza mbele ya vyombo vya habari juu ya kuwapo kwa zawadi nono.

Watasema habari njema wakijitakasa kwamba msimu huu mambo ni shwari na zawadi ni za kutakata. Hata hivyo, kwa bahati mbaya huwa ndivyo sivyo.

Huu si mpango mzuri kutokana na ukweli kwamba kama ulaghai huu hautapigiwa kelele, ipo siku yatakuja mabaya zaidi na hivyo kuondoa maana nzima ya kuwa na michuano ya aina hiyo.

Lakini pendekezo la Mwandika Busati ni kwamba wakati mawakala wa urembo wenye damu ya kidhalimu wakipigiwa kelele, ni vema washiriki wakawa mstari wa mbele kusema kwamba kuna uvundo ndani yake.

Wakinyamaza na kuacha yapite maana yake ni kwamba mizizi itazidi kupata nguvu na hivyo kukomaza ufisadi katika sanaa hiyo.

Kina dada washiriki wawe mstari wa mbele kukataa udhalilishwaji kama utajitokeza kambini. Hali kadhalika wakinusa rushwa ya ngono wainue ndimi zao na kusema na wala wasikae kimya.

Na kwa kufanya hivyo, idadi ya wahuni katika urembo watapungua kama si kutokomea kabisa.

Mwandika Busati anafikia ukomo. Anajituliza akiangalia neema zinavyomshukia kama mvua za masika zinazoendelea.

Wanaosema kuwa huu ni mwaka wa shetani wafikirie mara mbili mbili. Wanaweza pia kujitakasa kwa maji ya bahari ili kuondoa nuksi.

Wasalaam,

No comments: