Wednesday, December 29, 2010

Ni uhuru upi tunaojivunia?

Na Innocent Munyuku

MAMA Teresa wa Calcutta aliwahi kusema: “Yesterday is gone. Tomorrow has not yet come. We have only today. Let’s begin.” Mtawa huyo wa Kanisa Katoliki alizaliwa Agosti 26, 1910 na kufariki dunia Septemba 5 mwaka 1997.

Kwa tafsiri isiyo rasmi, Mama Teresa alikuwa akisema kuwa “Jana imepita. Kesho haijawadia. Tunayo siku ya leo. Tuanze kuifanyia kazi.”

Nimeanza makala haya kwa nukuu hiyo kutokana na malalamiko ya baadhi ya viongozi wa Serikali ya Tanzania na watendaji wengine wakuu pindi wanapoulizwa nini hasa kiini cha umasikini wetu hata baada ya kupewa uhuru miaka 49 iliyopita.

Wengi wao watatoa sababu zinazofanana. Watawataja wakoloni ama biashara ya utumwa kwamba ni mambo yaliyochangia umasikini wetu. Hapa wanaizungumzia JANA badala ya kuifanyia kazi LEO waliyonayo mkononi. Pengine itoshe kusema kuwa kuendelea kulalamika wakati huu tunapotimiza miaka 49 ya Uhuru wa Tanganyika ni ukosefu wa akili timamu.

Ninachotaka kusema hapa ni kwamba binafsi ninapotafakari uhuru huu, siamini kama kweli tuko huru. Huu ni sawa na uhuru wa bendera! Tanzania haiko huru kiuchumi na ndiyo maana watu wake wamelala kwenye dimbwi la umasikini.

Tanzania pamoja na kuwa na rasilimali nyingi, wananchi wake wanaendelea kutaabika. Mlo mmoja kwa siku ni jambo la kawaida kwao. Kwa mamilioni ya watu ndani ya ardhi hii kwao huo ndio mtindo wanaostahili na wanaishi sasa wakiwa na mazoea hayo.

Wajanja wachache wamejinufaisha na utajiri wa taifa hili. Tuliowapa dhamana ya kutufikisha katika nchi ya ahadi wametugeuka na kutuacha nyikani. Mali zinachumwa na kuliwa na hao wachache. Nyuso zao zimejaa furaha na wala hawana mawazo ya kuwaibua wengine. Labda watafanya hivyo kwa mtoto wa mjomba.

Hoja yangu ni kwamba sioni mantiki ya kusherehekea siku hii pasipo kwanza kufuta au kuwaangamiza watu wachache wanaosababisha mamilioni ya Watanzania wakose neema kwenye ardhi yao. Hatutakuwa huru kama tumebanwa na minyororo ya ufukara kiasi hiki.

Hao waliosababisha tukaingizwa katika mikataba mibovu inayotugharimu fedha nyingi wasiachwe wapite hivi hivi. Waliobariki mikataba ya hovyo kwenye madini ama vitalu vya uwindaji nao wawajibishwe ili walau keki hiyo iwasaidie Watanzania wengine. Vinginevyo sioni sababu ya kutamba kwamba tuko huru wakati kiuchumi hatuko huru.

Mara kadhaa ninapopata nafasi ya kuketi vijiweni na Watanzania wenzangu hasa vijana nanasa mambo mengi ambayo natamani mtawala wa nchi pia angepata wasaa wa kuyasikia. Bila shaka anayapata lakini kwa vile sina uhakika ni heri nitumie nafasi hii kuyasema baadhi ya masuala yanayojadiliwa kila wakati huko mitaani.

Leo hii Watanzania wanatimiza miaka 49 tangu wapate uhuru kutoka mikononi mwa Waingereza mwaka 1961. Ni sherehe kubwa na yenye simulizi nyingi; mbaya na njema. Miaka 49 ya uhuru si lele mama. Hii maana yake ni kwamba kama ni maisha ya binadamu Tanzania tayari ni mtu mzima anayejitegemea kwa mambo mengi. Si mtu wa hovyo!

Lakini kwa bahati mbaya sana miaka hii ya uhuru ni dhahiri kwamba hakuna jema la kujivunia ukilinganisha na mataifa mengine yaliyopata uhuru baada ya Tanzania. Sisi tumebaki kujisifu kuwa tuna amani.

Amani si jambo baya hata kidogo katika jamii, lakini amani wakati tumbo ni tupu, halina chakula ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu. Kinachosemwa mitaani ni kwamba Tanzania licha ya kuwa taifa huru, maisha ya Watanzania yameendelea kuwa magumu kila uchao.

Watu wanalalama kuhusu kupanda kwa bei za bidhaa hasa zile zinazohitajika katika maisha ya kila siku. Hicho ndicho wanacholalamikia. Lakini pia wanasema juu ya uwajibikaji mdogo wa watendaji wa Serikali. Wanazungumzia ubovu wa baadhi ya mawaziri, wakuu wa mikoa na wilaya.

Ingawa wengi wao hawana ubavu wa kupaza sauti, wanasema kwa kadiri wawezavyo kwamba hata watendaji katika ngazi ya vijiji ni waovu wasiopaswa kukalia viti hivyo. Hawaishii hapo, wanakerwa na ubovu wa huduma za afya. Kina mama na watoto, wazee na wahitaji wengine wa huduma hiyo wanakwazwa na utendaji wa wauguzi na madaktari.

Ninaamini kwamba hili halihitaji mjadala mrefu kwani hospitali na zahanati nyingi mambo si shwari kwa wagonjwa. Ni jambo la kawaida kwa wagonjwa kulala wanne kitanda kimoja. Hili si la ajabu. Si jambo geni pia kuwakuta wagonjwa wamerundikana chini wakilalia mkeka. Watanzania wamezoea. Si kama wameridhika bali mfumo umewaweka hapo.

Ukitaka muhuri wa Mtendaji wa Serikali za Mitaa nao siku hizi umekuwa mradi mkubwa kwa hao wenye dhamana ya kuushika. Karatasi haigongwi pasipo rupia mkononi. Wananchi wamezoea kulipa fedha hata kwa yale ambayo wanapaswa wahudumiwe bure. Yanaonekana kama vile yameshakuwa sugu na yasiyoweza kufutwa.

Si hi hayo tu, rushwa nayo ni keo kubwa kwa Watanzania. Wengine wamefikia hatua ya kusema kuwa kama kuitokomeza imeshindikana, basi tuihalalishe. Watu wanakwenda kwa mtindo wa kisasa na kutokana na hali hiyo si rahisi leo hii kuwanasa wala rushwa kama ilivyokuwa miaka 10 iliyopita.

Pamoja na ukweli kwamba wananchi wana mchango mkubwa katika kukabiliana na rushwa, wanacholalamikia wao ni kwamba walio juu ndio viongozi wa jambo hilo. Wanasema kama katibu mkuu wa wizara anadaka rushwa mwananchi wa kawaida afanyeje? Tule wote kwani huo ndio mpango uliopo.

Wengine wananong’ona kwamba kama mbunge fulani kaingia bungeni kwa njia ya hongo diwani naye ataachaje kutetea nafasi yake kwa rushwa? Haya si mambo ya siri yanasemwa lakini kwa bahati mbaya sana si rahisi kuyapatia ushahidi. Lakini ukweli wa mambo ni huo rushwa inanuka nchini.

Hii maana yake ni kwamba walio wengi hawapati huduma kwa kiwango kinachostahili. Kama ni ajira, matibabu na mengine hayapatikani mpaka utoe rushwa. Ukikanyaga polisi utaambiwa hawana karatasi ya kuandikia maelezo ya mlalamikaji. Lakini kabla ya hilo kama utakuwa unahitaji kuwapeleka mahala alipo mtuhumiwa utaelezwa kwamba hawana gari na kama lipo watasema halina mafuta. Kodi tunazolipa zinatumikaje?

Hizo zote ni njia za kukufanya uwe mstari wa mbele kufungua pochi na kuwapa ulichonacho ili mambo yaende. Hii ndiyo miaka 49 ya Uhuru wa Tanganyika tunayoishi. Kwa uwazi ni kwamba maisha ya rushwa hayana maana nyingine zaidi ya kuendelea kukandamizana na kwa njia hiyo kuliangamiza taifa.

Kama nilivyodokeza awali, kuna waliodiriki kusaini mikataba hafifu ya kimataifa ambayo leo hii taifa linaangamia kwa kukosa maarifa. Waliopewa dhamana wamekula cha kwao na hawana hofu ya maisha. Anayepata taabu ni mlalahoi ambaye hajui aanzie wapi ili afikie kilele cha maisha bora. Amekwazwa na mfumo ambao hautaki mabadiliko.

Hayo ndiyo yanayosemwa vijiweni lakini hakuna shaka kwamba ndiyo hali halisi kwa maisha ya kila siku. Je, katika miaka 49 ya uhuru Watanzania tunajivunia nini? Imani na utulivu wa kutoona mabomu yakilipuka mitaani? Pengine yapaswa kuwapo na tafakuri ya kina kwani kwa mtazamo wangu amani kamili maana yake ni kuwa na utulivu wa akili pia.

Kama matumbo hayana shibe sidhani kama mtu anaweza kutembea kwa matao akisema kuwa yu huru na amani ya kweli. Tusibweteke na miaka 49 ya uhuru tusake njia ya kujikwamua uwezo tunao. Wenye mamlaka ya kuwaongoza wananchi waache visingizio, tuache kuijadili JANA badala yake tuifanyie kazi LEO.

munyuku@gmail.com
0754 471 920

Imani kisiwe chanzo cha umasikini

Na Innocent Munyuku

BIBLIA Takatifu katika kitabu chake cha Waebrania mwanzoni kabisa inatoa maana ya neno ‘imani’. Kwamba imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.

Katika Waebrania 11: 3 imeandikwa kuwa kwa imani twafahamu ya kuwa ulimwengu uliumbwa kwa neno la Mungu, hata vitu vinavyoonekana havikufanywa kwa vitu vilivyo dhahiri.

Kwa jumla sura yote ya 11 katika kitabu hicho cha Waebrania inaelezea imani ilivyofanya kazi kwa watumishi tele wa Mungu kama vile Nuhu, Henoko, Ibrahimu, Sara, Yakobo na Musa.

Aghalabu binadamu wengi kama si wote tuna imani na jambo fulani katika maisha yetu ya kila siku. Ndiyo maana pahala pengine husemwa kuwa imani inaweza kuhamisha milima.

Suala la imani wakati mwingine ni gumu sana. Kwa mfano, si rahisi kwangu binafsi kuniaminisha dini nyingine tofauti na ninayoiamini. Itamchukua mtu muda mrefu kunishawishi ili niingie katika kundi lake. Haya ni matokeo ya imani.

Binafsi naamini kwamba dunia na vyote vilivyomo vimeumbwa na Mwenyezi Mungu. Hata hivyo, wapo wengine hawaamini hivyo.

Hapo juu nimedokeza kuwa ni vigumu kwa mmoja kumshawishi mwingine kuamini anachokiamini yeye. Hilo ni jambo gumu na hushauriwa pia kuwa si busara kuingilia imani za watu wengine.

Hata hivyo, katika makala yangu haya leo naomba kuingilia imani za wengine si kwa shari bali kwa lengo la kujenga umoja na misingi bora ya maendeleo.

Katika miaka ya hivi karibuni, kumeibuka makanisa mbalimbali nchini. Kuibuka kwa makanisa hayo kumeibua pia watu wanaojipachika kuwa ni ‘manabii’, ‘maaskofu’, ‘mitume’ na ‘wachungaji’. Idadi yao ni kubwa na inaendelea kupanuka kila leo.

Mafundisho katika makanisa hayo, baadhi yanajenga na mengine yanabomoa ujenzi wa jamii huru ya Tanzania. Yapo makanisa yanayowalazimisha waumini wake kutoa sadaka au zaka kwa kiwango fulani cha fedha ili wabarikiwe na Mungu. Haya yanatendeka!

Mafundisho kama haya sidhani kama yanalenga kumwinua muumini huyo kutoka katika lindi la umasikini. Badala ya kuwekeza unatoa kila kilicho chako na kulala njaa kwa imani kwamba utashushiwa baraka kutoka juu.

Wengi wao pia wameacha kufanya kazi viwandani, ofisini na kazi nyinginezo za kujiingizia kipato na badala yake wameamua kushinda makanisani wakiamini kwamba kuna miujiza itashuka.

Naomba kusema kwamba tabia ya aina hii si ya kufumbiwa macho na kwa upande mwingine kuna haja kwa mamlaka za juu serikalini kuangalia mienendo ya makanisa haya.

Kuyafumbia macho ni hatari kubwa kwa taifa la Tanzania. Si ajabu siku moja yakatokea ya nabii wa uongo, Joseph Kibwetere wa Uganda ambaye kwa sasa ni marehemu.

Kibwetere aliitingisha Uganda mapema miaka ya 1990 baada ya kudai kuwa alikuwa akitokewa na Bikira Maria. Kibwetere kwa ushawishi mkubwa pamoja na Credonia Mwerinde wakaunda kanisa kubwa lililovuta watu wengi. Baadaye wakatangaza kuwa mwaka 2000 ulikuwa mwisho wa dunia. Kilichotokea ni kwamba mamia ya waumini hao waliangamizwa wakiwa katika kile kilichoitwa kuwa ni ibada takatifu.

Tukio hilo lililotokea Machi 17 mwaka 2000 katika Kijiji cha Kanungu nchini Uganda lilileta mpasuko wa roho kwa watu wengi.

Ninachojaribu kusema ni kwamba wimbi hili la kuibuka kwa makanisa linadhibitiwa vipi? Je, Serikali inafuatilia kwa makini mafundisho ya makanisa hayo? Hata kama Serikali haina dini, nadhani upo lazima wa kuweka udhibiti ili jamii ya wazalishaji isipungue.

Binafsi napata shaka kidogo ninapowaza kuibuka kwa mambo kama haya. Sisemi kwamba watu wasisali. La hasha! Ninachosema ni kwamba kuwe na mpango maalumu wa kufuatilia mafundisho na mienendo ya hao wanaojiita manabii.

Mfano hai, jijini Dar es Salaam, yupo kijana mmoja anayejiita ‘Nabii Tito’ anapita mitaani hasa sehemu zenye baa akihubiri na Biblia yake mkononi. Mafundisho anayoyatoa ni ya upotoshaji kabisa.

Kwa mfano hasiti kusema kuwa mwanamume sharti awe na wanawake wengi na kwamba wakati wa kujamiiana asitumie kondomu. Pia anahamasisha unywaji wa pombe kupita kiasi na uvutaji wa sigara. Je, mtu wa aina hii kwanini anaachwa akitamba na mafundisho ya kihuni namna hii?

Leo hii, Yesu amegeuzwa kuwa kitega uchumi. Mtu mmoja anaibuka asubuhi na kujitangaza kuwa ni ‘nabii’ na kisha kuwatia hofu waumini wao. Waumini hao wataacha kujenga familia zao na kukimbilia kujenga familia ya ‘nabii’.

Waumini hao kwa vile wameamua kuachana na kazi za kusaidia familia zao, wamebaki kama makinda ya ndege wakisubiri miujiza kutoka kwa Mungu. Imani ya aina hii ni hatari kwa ujenzi wa taifa letu.

Michango tele makanisani, njaa kali huko nyumbani. Huo ndio utamaduni wa sasa. Nadhani huu ni wakati wa mabadiliko. Tusiache Watanzania wakiyumbishwa katika imani ambazo mwishowe zitaligharimu taifa. Huu ndio mtazamo wangu.

munyuku@gmail.com

Mlikuja kuomba uwaziri au ubunge?

Na Innocent Munyuku

WAMAKONDE wana msemo: “Chimfaa munu amaa mwene.” Kwa Kiswahili unaweza kusema kuwa ‘Kimfaacho mtu anajua mwenyewe mhusika.’

Kwamba usishangae mwanamume mwembamba kupenda mwanamke mnene au mwanamke mrefu akapenda mwanamume mfupi. Au mwingine akapendelea kula maharage mara kwa mara na kuacha kula nyama licha ya kuwa ana fedha za kutosheleza kitoweo. Hayo yote ni matakwa na ridhaa ya mhusika.

Uchaguzi Mkuu kwa mwaka huu umeshamalizika tangu Oktoba 31 na tayari Rais Jakaya Kikwete yupo Ikulu kutimiza kiapo cha kuwatumikia wananchi. Hali kadhalika wabunge na madiwani nao wameshajulikana.

Wakati wa kampeni, kila mgombea alikuwa akinadi sera zake kwa mgongo wa chama chake cha siasa. Wananchi wakasilikiliza kwa makini na hatimaye kufanya uamuzi wa nani apigiwe kura za NDIYO.

Walipokuwa majukwaani kueleza sera zao na kuomba kura, wapigakura kila mmoja kwa wakati wake alikuwa na chaguo binafsi. Kwamba kila aliyepiga kura naamini wengi wao lilikuwa suala binafsi.

Sidhani kama kuna aliyepigwa kura kwa shinikizo bali kwa ridhaa kwani aliamini kuwa mgombea atakayefaa kumwongoza ni fulani na hapo ndipo unapogota kwenye msemo kwamba kimfaacho mtu anajua mhusika mwenyewe.

Leo hii ukiwauliza wapigakura hao matarajio yao kwa mbunge watakupa mambo tofauti tofauti lakini hoja zao zote zitasimama katika lugha moja tu yaani maendeleo katika jamii husika.

Naam! Maendeleo kwani ndicho hasa kilichowasukuma wengi wakaamua kumpa mgombea fulani kura za NDIYO naye akapata kuwa mwakilishi wa jimbo kule bungeni.

Pamoja na ukweli kwamba kuna zumari lilipigwa kuhusu udini na ukabila, sidhani kama wagombea wengi walioibuka kidedea wanazama katika dimbwi hilo la kipuuzi. Ninachoamini ni kuwa wapigakura wengi waliamua kumpa fulani nafasi ya kuwa mbunge kutokana na sera zake.

Kama kuna waliompa kura mgombea kwa kigezo cha udini au ukabila hao ni mabahau. Mabahau wakati mwingine huitwa mazuzu. Kwa ujumla ni aina ya watu ambao ni sawa na majuha.

Mwishoni mwa Novemba mwaka huu, Rais Kikwete alitangaza Baraza la Mawaziri. Kabla ya kutangazwa kwa baraza hilo, kama ilivyo kawaida, wananchi wa kada mbalimbali walikuwa wakisubiri kwa hamu muundo wa baraza hilo jipya kwa maana ya nani atakuwa wapi.

Baadhi ya wabunge na mawaziri wa zamani wakawa tumbo joto kwani hawakujua hatima yao katika baraza lijalo. Hatimaye Rais Kikwete akavunja ukimya na kuyaweka hadharani majina ya mawaziri wake.

Baada ya baraza jipya kujulikana, mitaani kuna minong’ono kwamba baadhi ya wabunge hawajaridhika kwani walikuwa na matarajio makubwa ya kuwa miongoni mwa baraza jipya la Kikwete. Mbali na baadhi ya wabunge kusononekea mafichoni, wapo wapambe wao wanaoamini kuwa ‘mtu wao’ kafanyiwa hila!

Hili ni la kushangaza sana. Binafsi nashangaa hadi kuhisi kuchefuka. Nashangaa kwa sababu mbunge huyo au wabunge hawa walipokuwa wanapanda jukwaani kuomba kura sikupata kumsikia au kuwasikia wakiomba kura za kuwa mawaziri.

Walipanda jukwaani kuomba ridhaa ya kwenda kuwa wawakilishi kule bungeni ‘mjengoni’ mjini Dodoma. Kwanini basi leo hii msononeke kwa kutokuwamo katika Baraza la Mawaziri?

Mlikuja majimboni kwa unyenyekevu mkamwaga sera tamu za kuinua maendeleo ya wananchi. Mkapigiwa kura na baadhi yenu mmepita kwenye tundu la sindano. Leo hii mnaanza kulalamika kwa kukosa uwaziri. Je, huu si ndio uwendawazimu?

Ndiyo maana nikaona ni heri nitumie nafasi kuwatwanga swali kwamba hivi mlikuja majimboni kuomba kuwa wabunge au mawaziri?

Kama mlikuja kuomba kura za kuwa wabunge kwa maana ya wawakilishi wetu katika Bunge, basi timizeni majukumu yenu kwa mujibu wa makubaliano na wapigakura.

Makubaliano hayo ni mkataba au kitanzi chenu. Kwamba hakikisheni mnatimiza ahadi zenu. Kama uliahidi kumalizia ujenzi wa daraja fanya hivyo. Chakarika, tafuta fedha ziliko timiza ahadi yako.

Utakuwa mwakilishi wa ajabu sana kama utaendelea kulalama kwamba Rais Kikwete kakutenga. Ulikuja jimboni kuwa mbunge na wala hakuna siku ulitamka kuutaka uwaziri.

Tanzania yetu hii, kama nilivyosema katika safu hii juma lililopita, ni nchi tajiri lakini mbali na kuachwa huru na Waingereza mwaka 1961, taifa limekuwa likididimia. Kisa? Watendaji wakuu hawana uzalendo.

Mtu haoni soni kuingia mkataba mbovu ambao kesho yake unaliumiza taifa. Si mara moja au mbili tumesikia kuwa ‘mkubwa’ fulani katumia vibaya fedha za wafadhili ambazo kimsingi zililenga kuleta maendeleo kwa jamii.

Angalia leo hii matumizi makubwa serikalini. Walau Waziri Mkuu Mizengo Pinda anaonyesha njia. Ameshakataa kupewa gari jipya lenye thamani zaidi ya Sh milioni 200. Huyu ana moyo wa kizalendo.

Lengo langu ni kuonyesha kuwa kama kuna mbunge leo hii analalama kuachwa kwenye Baraza la Mawaziri, maana yake ni kwamba huyo hana nia ya dhati ya kuwatumikia wananchi. Huyo kwa vijana wa mjini ataitwa ‘mpiga dili’.

Kiongozi wa aina hiyo ambaye haguswi na umasikini wa watu wake na badala yake kuota ndoto za kuwa waziri ni wa kuogopwa. Naapa miaka mitano si mingi itafika siku naye ataliangalia Bunge kwenye video.

Nihitimishe kwa kusema kuwa huu si muda wa kulilia uwaziri, tenda uliyowaahidi wananchi kule jimboni kwako na huo ndio uungwana kwani hata wa kale walisema muungwana kwake ni vitendo. Timizeni ahadi.

munyuku@gmail.com
0754 471 920

Anguko la CCM haliko mbali

Na Innocent Munyuku

KESHO Ijumaa tunahitimisha mwaka 2010 na kuingia mwaka mpya wa 2011. Kwa watakaobahatika kuuona mwaka mwingine hawana budi kumshukuru Mungu.

Mwaka huu unaogota kesho ulikuwa na mambo mengi. Mipango ilikuwa mingi na bila shaka kuna mengi pia yametekelezwa huku mengine yakitelekezwa.

Binafsi nauangalia mwaka 2010 kwa jicho pana hasa katika ulingo wa siasa. Pilika zilikuwa nyingi kutokana na ukweli kwamba mwaka huu tumefanya uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani.

Uchaguzi wa mwaka huu tumeshuhudia maajabu makubwa. Wananchi sasa wameanza kubaini nini kinawafaa. Wako huru kuchagua wanachokitaka. Zile nyakati za hofu zimekwenda na maji na ndiyo maana Chama Cha Mapinduzi-CCM kimepata wakati mgumu safari hii.

Hakuna anayeweza kubisha hilo. Angalia matokeo katika majimbo ambayo awali yalionekana kuwa nguzo muhimu ya CCM, leo hii yameangukia Upinzani. Wananchi wametumia haki yao na kufanya uamuzi.

Kimbunga cha safari hii ni ishara tosha kwamba miaka ya CCM kucheza na akili za watu zimekwenda na maji. Enzi za kuwalaghai wapigakura kwa vipapatio vya kuku na fulana zinaelekea ukingoni.

Kichwa cha habari cha makala haya kinasema: ‘Anguko la CCM haliko mbali’. Naam, huo ndio mtazamo wangu. Kwamba kwa mwenendo wa chama hicho hivi sasa kama hakitakubali mabadiliko chanya basi huo ndio mwisho wao.

Nasema hivyo kutokana na ukweli kwamba baadhi ya watendaji wakuu wa chama hicho ni kama vile wamelewa madaraka. Baadhi yao hawaambiliki, hawataki kukosolewa. Wameamua kuishi kwa mazoea! Hilo ni kosa kubwa katika utawala.

Pengine hayo yanatokea kwa vile katika uso wa dunia, mwanadamu kapewa akili inayomwezesha kupangilia mambo mbalimbali maishani mwake.

Hata hivyo, husemwa kwamba akili ni nywele kila mtu na zake. Hii maana yake ni kwamba si rahisi mkafanana mawazo na ndiyo maana katika jamii huzuka mijadala ya mabishano.

Lakini kwa kutumia akili hiyo hiyo binadamu amekuwa fundi au mahiri wa kugeuza mambo fulani. Mtu mwenye ukurutu kwa mfano atajitahidi kuficha maradhi hayo kwa kuvaa gubigubi.

Hali kadhalika kwa mwenye mapunye kichwani haishangazi akionekana na kofia au kilemba. Hizo zote ni mbinu za kuficha maradhi hayo mbele ya wengine.

Lakini kuna mengine hayafichiki kama vile chongo. Si dhambi nikawakumbusha viongozi wa CCM kwamba wanjamanga si dawa ya chongo. Si rahisi kuficha kilema.

Nani hajui kuwa leo hii ndani ya CCM kuna mpasuko? Kila kukicha baadhi ya makada wa siku nyingi wamekuwa wakirushiana maneno ambayo kimsingi hayalengi kukiimarisha chama.

Kila mmoja ndani ya chama sasa anayo nafasi ya kupayuka na kutoa hisia zake. Hii ni dalili ya wazi kuwa humo ndani kuna fukuto. Tanuru linawaka na kwa mtindo huo, Wana-CCM sasa wanajikaanga kwa mafuta yao.

Vurugu kwenye kura za maoni ni ushahidi mwingine kwamba CCM sasa inaporomoka. Wengi wetu tumeshuhudia maajabu katika mchakato mzima. Baadhi ya majimbo yameangukia kwa wapinzani kutokana na CCM kucheza karata zisizo.

Mgombea wao anashinda kura za maoni, lakini mwishowe anawekewa zengwe zenye pembe. Hila za aina hiyo zimeiponza CCM kwa kiasi kikubwa.

Kwa mtazamo wangu, CCM inahitaji mabadiliko makubwa. Vinginevyo utabiri wangu hakika utatimia. Kwamba huu ni mwanzo wa mwisho mwa CCM. Bila shaka chama hicho sasa kinahitaji fikra pevu. Vijana wapewe nafasi, wazee wabaki kuwa washauri pale inapobidi.

Marehemu Profesa Haroub Othman aliwahi kusema kuwa ule mtandao wa CCM mwaka 2005 ulikuwa wa kihistoria lakini wahusika hawakujua nini cha kufanya mara baada ya kumweka mtu wao katika madaraka ya urais.

Kwa mujibu wa Profesa Othman, wanamtandao walileta mapinduzi ambayo katika Afrika hayakuwahi kutokea. Kwamba walijipanga vema kumwinua mgombea wao, wakamnadi kwa udi na uvumba na wakafanikiwa kumpeleka Ikulu. Lakini baada ya hapo wakaanza kugawana fito!

Kama mtandao ule ungekuwa na fikra pevu, leo hii Tanzania isingekuwa nchi ya kulia na matatizo haya yanayotukabili kama vile mgao wa umeme, shida ya maji, mfumko wa bei na mengi yafananayo na hayo.

Lakini tumefika hapa kwa sababu ya vurugu za wao kwa wao. Hawakujipanga kuleta mageuzi ya kudumu. Kila mmoja aliingia na lake jambo. Ulikuwa kama mchezo wa kuviziana.

Inashangaza sana leo mmoja wa wanachama anakemea vurugu na kuhimiza majadiliano kwa ajili ya maelewano halafu mtendaji wa chama anaibuka kusema kuwa CCM haihusiki na vurugu na kwamba hakuna haja ya majadiliano. Hili ni la kustaajabisha.

Hamkani tena kwamba ndani ya CCM leo hii, hakuna wa kumwamini mwenzake. Kila mmoja anakwenda kwa hadhari kubwa kwani hajui mwenzake ana silaha gani. Chai hainyweki kama zamani kwa sababu hujui mwenzako ana jambo gani moyoni.

Salamu sasa ni za mdomoni na wala si za kutoka rohoni kama enzi za Mwalimu Nyerere na Rashid Kawawa. Leo hii, CCM wanaogopana, wanaviziana. Kwa mtindo huo chama hakiwezi kufika mbali.

Narejea kusema kuwa huu ni utabiri wangu kwamba anguko la CCM haliko mbali. Siku za CCM kuitwa chama cha Upinzani ziko jirani ni suala la kusubiri tu.

Nihitimishe makala yangu kwa kuwatakia kila jema katika mwaka mpya wa 2011.

munyuku@gmail.com