na innocent munyuku
HERI ya Krismasi na fanaka ya mwaka mpya wa 2008. Mzee wa Busati anaimba Haleluya akila vipapatio vya kuku kwa pumzi yenye rutuba ambayo Mola amemjalia.
Yamekuja mengi mabaya na mazuri lakini kwa sasa neema imefika mlangoni. Kaya yake inadunda kwa mema. Hakuna matata.
Wiki hii Mwandika Busati kama ilivyo ada anakuja na porojo zake lakini zilizojaa udadisi na changamoto kwenye bongo za Wadanganyika.
Wiki hii Mwandika Busati ameamua kuwa tofauti na fikra za Wabongo walio wengi hasa kwa wapenda soka nchini.
Linalosemwa na Mzee wa Busati ni hali ya timu ya taifa ya Tanzania Bara ambayo wiki msimu huu kwa mara nyingine imeshindwa kubeba Kombe la Chalenji.
Kocha Mkuu wa timu hiyo Marcio Maximo kwa sasa bila shaka hawezi kutembea mitaa ya Kariakoo kama ilivyokuwa miezi sita nyuma.
Hawezi kutembea kwa matao kwa sababu watu wamefura. Wanachosema ni kwamba Maximo hawezi tena kuwa kocha wa timu hiyo. Kisa? Timu yao imefanya vibaya kwenye michuano hiyo.
Walitamani kombe libaki nyumbani na bila shaka hiyo ingekuwa zawadi mwafaka kwa Noeli na Mwaka Mpya. Lakini ndoto hiyo imekuwa chungu.
Kinachosemwa kwenye vijiwe sasa ni kwamba Maximo kashindwa kazi na kilichobaki afungashe aende zake Brazil.
Lakini Mzee wa Busati angependa hoja ya kumbeza Maximo sasa iwekwe kando kwa sababu ukweli wa mambo ni kwamba bado Tanzania haijasukwa vema katika soka.
Wakati fulani Mwandika Busati alipata kusema kuwa wanaopiga kelele kwamba Maximo hafai bila shaka ni wendawazimu kutokana na historia ya soka nchini.
Maximo kutoka Brazil ambako wanavuma katika soka haina maana kwamba angeweza kuibadilisha soka ya bongo kwa siku moja. Angali anahitaji muda.
Leo hii mwapiga kelele kwamba hafai, waliokuwapo kabla ya Maximo walitenda nini jema katika soka ya Tanzania? Si waliishia kupiga soga na kulumbana kila kukicha?
Mwasema ati Maximo hashauriki. Nani aliwahi kumshauri naye akagoma kufuata kilichosemwa?
Mwanena pia kwamba ati mlijua Maximo hana lolote. Huu ni unabii ambao kimsingi hauna tija katika maslahi ya soka nchini. Aliwakuta wachezaji wameshakauka hata akijaribu kuwakunja wanameguka. Huo ndio ukweli wa mambo.
Mwacheni apange timu awezavyo. Kumrushia madongo ya lawama ni kutomtendea haki kwani wengi wenu bila shaka mwaelewa matatizo ya huko nyuma.
Mzee wa Busati kwa kawaida hafichi kuweka wazi misimamo yake. Hata kama anaona kufanya hivyo kunaweza kumtenga na masahiba zake hilo kwake halimpi shida.
Maximo si wa kulaumiwa. Jiulizeni tuliteleza wapi na Maximo anajaribu kufanya nini.
Kama Mwandika Busati haendi mbali na ukweli ni kwamba anachofanya Maximo kwa sasa ni kutengeneza pepo ya soka kwa miaka ijayo.
Mnaodhani leo hii mtabeba Kombe la Dunia ni kupoteza wakati kwani hilo kimsingi haliwezakani. Acheni porojo mwacheni Maximo na programu yake.
Vinginevyo Mzee wa Busati anawapa uhondo wa shairi ambalo katumiwa na sahiba yake anayekwenda kwa jina la Mwafrika Merinyo. Kila la heri!
Sikukuu ziwe na raha
Zisijewepo karaha
Sote tuombe furaha
Na ucheshi na mizaha
Tule tunywe kwa staha
Ituwakie ya jaha!
Tumuombe na Karima
Tujalie yalo mema
Mwaka uishe salama
Heri isije tuhama
Tuondolee zahama
Riziki zisije zama!
Tufanyiane mazuri
Ya baraka na ya heri
Tujiepushie shari
Na fahari na kiburi
Tuzisafishe saduri
Mabaya tusihiyari!
Upendo kita mizizi
Heshima ikaze uzi
Vita tupige uozi
Tusije lia machozi
Ukweli nao uwazi
Ziwe ndo zetu hirizi!
Sinza kwetu karibuni
Mwaka huu na mwakani
Mavazi furahieni
Myavae maungoni
Kwa maarufu washoni
Msisahau jamani!!!!!!!!!!!
Wasalaam,
Wednesday, January 2, 2008
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment