Na Innocent Munyuku
KATIKA uso wa dunia, mwanadamu kapewa akili inayomwezesha kupangilia mambo mbalimbali maishani mwake.
Hata hivyo, husemwa kwamba akili ni nywele kila mtu na zake. Hii maana yake ni kwamba si rahisi mkafanana mawazo na ndio maana katika jamii huzuka mijadala ya mabishano.
Lakini kwa kutumia akili hiyo hiyo binadamu amekuwa fundi au mahiri wa kugeuza mambo fulani. Mtu mwenye ukurutu kwa mfano atajitahidi kuficha maradhi hayo kwa kuvaa gubigubi.
Hali kadhalika kwa mwenye mapunye kichwani haishangazi akionekana na kofia au kilemba. Hizo zote ni mbinu za kuficha maradhi hayo mbele yaw engine.
Lakini kuna mengine hayafichiki kama vile chongo. Mwanawane hata kama utapaka wanjamanga, chongo halifichiki kama lilivyo pembe la ng’ombe.
Mzee wa Busati kaibuka Jumanne hii ya ‘wajinga’ akiwa na hoja juu ya ukuzaji wa soka ndani ya Tanzania ambayo kimsingi ni kama vile wadau wanatwanga maji kwenye kinu.
Mengi yamekuwa yakisemwa kwa mbwembwe juu ya ukuzaji wa soka ndani ya bongo lakini ukweli wa mambo ni kwamba mbwembwe hizo ni danganya toto.
Kinachofanywa na viongozi katika mamlaka za soka ni sawa na kuficha chongo kwa kupaka wanjamanga. Porojo zimejaa kila mahala na ndimi zao zimejaa ushawishi wa giza.
Angalia msimu wa usajili unapowadia. Balaa mtindo mmoja. Viongozi wa klabu ndio wenye kimbelembele cha kuchagua wachezaji wanaodhani wataifaa timu yao.
Wanafanya hivyo bila kuwapa nafasi makocha katika suala la usajili. Matokeo yake ni kwamba si ajabu ukakuta timu haina beki mahiri kwa sababu pengine viongozi waliamua kuwajaza washambuliaji pekee.
Leo hii viongozi wa klabu wamekuwa kama miungu watu. Wengi wao hawana hata sifa za kuitwa viongozi wa soka. Hawafai waitwe hivyo kwa vile hawana taaluma ya mpira wa miguu. Wanachojua ni kupiga soka na kueneza ufitini.
Kwani hamjapata kusikia kuwa kiongozi fulani kaidhinisha adhabu kwa mchezaji pasipo sababu za msingi? Yanatokea kila leo na yangali yakiendelea.
Mwandika Busati anachosema ni kwamba kauli nyingi za zinazohubiri makuzi ya soka hazina maana kwa sasa kama mamlaka zinazohusika hazitaangalia kiini cha udumavu wa medani hiyo.
Haina maana kusema kwamba Wabongo wajipange kucheza fainali za Kombe la Dunia huku viongozi wababaishaji wasioweza hata kuchanganua mambo wakiendelea kukalia viti hivyo.
Anachonena Mzee wa Busati ni kwamba linapokuja suala la kukuza soka watoa hoja waangalie watokako, walipo na mwelekeo mbele yao.
Siku chache zilizopita, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Joel Bendera katoa mapendekezo yake katika mbio za kuboresha soka nchini.
Bendera amesisitiza umuhimu wa kuwashirikisha waamuzi na madaktari katika mafunzo ya soka. Kwamba wadau hao wapewe mafunzo ya mara kwa mara.
Huo ni mtazamo chanya unaungwa mkono na Mwandika Busati lakini bado ipo haja ya kuangalia magugu yaliyojaa ndani ya klabu mbalimbali za soka na vyama vyake.
Hatuwezi kuwa na mng’aro katika soka huku walioshika nafasi za uongozi wakiwa wapiga soga wasiokuwa na dira ya maendeleo.
Matokeo yake ni kwamba klabu nyingi zimebaki kuwa makaburi ya wachezaji kwa sababu viongozi wake wamekosa mwelekeo wenye neema. Hao kazi yao ni porojo na mahubiri ya ‘soka fitna’.
Kubebana na kuficha maradhi kwa kuvaa gubigubi hakutasaidia kwani ipo siku mambo yataharibika zaidi ya leo.
Leo hii bado kuna viongozi wa klabu za soka wanaoendelea kuamini ushirikina katika mchezo huo. Hawapeleki timu dimbani pasipo kuwalaza wachezaji makaburini au kuwanyoa nywele za kwapa.
Je, kwa sampuli hii ya uongozi mwadhani mtapaa kwenye ndege ya mafanikio ya soka? La hasha! Mtabaki kama mlivyo.
Mzee wa Busati hana budi kukunja jamvi. Ajiendee porini kwake kwa mapumziko akiamini kwamba somo limeeleweka.
Kwa walionaswa katika Siku ya Wajinga leo hii poleni kwa kujazwa ujinga. Vinginevyo muwe makini msimu ujao.
Wasalaam,
Sunday, March 30, 2008
Saturday, March 22, 2008
Hamkani baadhi mnaitumikia ngono
Na Innocent Munyuku
KUMEKUCHA! Mzee wa Busati katumbukia kwenye buti tayari kwa mwendo wa kila Jumanne. Kwake mambo yako sawia ingawa anaelewa kwamba wapo waliopata majereha kiduchu kwenye pochi zao wakati wa ufufuo wa Bwana Yesu.
Hata hivyo, uhai ungalipo pumzi ya Mola inashuka. Hata kama mlo ni wa shida hayo ni majaribu na mapito ambayo mwenye kutoka damu sharti akumbane nayo.
Kina Momburi bila shaka sasa wanatweta hawajui watafikaje Tabata Relini. Si mchezo papake Mwanyamala hadi Tabata kwa mguu! Yataka moyo mwanawane.
Bila shaka sasa wanatembeza bakuli wakitoa sera tamu tamu ili wapate kufika tarehe njema za mwajiri. Lakini analoomba Mzee wa Busati ni kwamba msije zua misiba ambayo haipo ili mpate ngwenje za matanuzi. Mkitenda hayo mtakosa thawabu.
Juma lililopita Mwandika Busati alinena juu ya ukakasi wa sanaa hasa ya maigizo na mchezo wa ngono katika eneo hilo.
Akaweka wazi kwamba baadhi ya vikundi hivyo vya maigizo hasa vinavyoonyesha kazi zao kwenye runinga vimekuwa na mchezo mchafu wa kuwalazimisha ngono kina dada (waigizaji) ili wapate nafasi ya kuonekana kwenye vioo vya televisheni.
Na moja ya aya katika makala hayo ya juma lililopita ilisomeka hivi: “Mambo kama hayo kwa hakika yanasikitisha na kutia kichefuchefu. Kwamba kama viongozi wa vikundi fulani vya sanaa wanafikia hatua ya kudai rushwa ya ngono hii ni aibu.”
Kuanzia mwanzo wa waraka huo wa hadi mwisho hakuna pahala Mwandika Busati ametaja kikundi fulani au jina la kiongozi anayeendekeza ukware.
Lakini cha ajabu akaibuka mtu mmoja aliyejiita kiongozi wa kikundi cha sanaa za maigizo na kumtuhumu na kisha kumhukumu Mwandika Busati kwamba hakufanya kile yeye alichokiita ‘research’.
Akahitimisha hivyo kwamba katika sanaa ya maigizo mambo hayo hayapo. Mzee wa Busati naye akapata wasaa wa kuuliza iweje aitwe mdanganyifu?
Hiyo njemba ikadai eti kwa vile sikuwapa nafasi viongozi kupata maoni yao!(?). Akasisitiza hilo kwamba sikuwahoji viongozi wa makundi kisa Mzee wa Busati hakufika kwake!
Yeye ni nani hadi alazimishe kufikiwa? Pengine angesema kwamba yeye ndiye kinara wa viongozi wa vikundi vya sanaa nchini basi hoja yake ingekuwa inaelekea kwenye ukweli.
Kwani ni lazima kila kile alichokiita ‘research’ afikiwe kila mmoja? Twaangalia uwingi wa matukio na kama yeye hafanyi hivyo basi Muumba amrehemu.
Lakini ukweli wa mambo ni ule ule kwamba HAMKANI ndani ya sanaa kuna baadhi ya matukio ya kulazimisha unyumba ili binti fulani apate nafasi
Hata katika baadhi ya filamu za Kibongo nako ni kama shambiro kwa maana ya sehemu ambayo hufanyika mambo ya hovyo hasa yahusuyo ukahaba au uhuni ufananao na huo.
Mwandika Busati alitarajia kwamba jamaa aliyejiita kiongozi wa kundi la sanaa la maigizo angeleta hoja ya ushirikiano ya kukemea hali hiyo na si kushutumu na kisha kuhukumu kwamba Mwandika Busati hajui alichokinena.
Leteni hoja mezani tusemezane na si kujitakasa kwa maji ya bahari.
Haya si mashambulizi la hasha! Kinachosemwa na Mwandika Busati ni kwamba yafaa wakati mwingine kujadili ndani ya nafsi kabla ya kupayuka kwamba fulani katema urongo.
Au mpaka siku zipigwe kura za siri ndipo mpate kusadiki yasemwayo na Mzee wa Busati? Mwandika Busati aseme uwongo ili iweje?
Mlitaka asiseme ili iweje? Nanyi kuweni wadadisi na hakika mtayabaini haya kwamba yapo baadhi ya makundi ambayo hongo ya ngono imetawala.
Ndio maana juma lililopita ikawekwa wazi kwamba hawa si wasanii kwa sababu wameingia humo kiufisadi. Wamevaa joho lenye udhalimu ndani yake.
Habari ndiyo hiyo kwamba haya yasemwayo yapo na yanaendelea kufanyika. Kukaza koo na kusema kwamba fulani kasema uwongo bila shaka ni kutotenda haki.
Mzee wa Busati amefikia ukomo kwa juma hili akitaraji maoni kutoka kwa wadau.
Lakini jambo moja lililo wazi ni kwamba yu radhi hata ikibidi kupigwa mawe akitetea hoja yake. Hakuna urongo hapa. Wasanii wengi wa kike ni mashuhuda na haya.
La maana ni kuangalia namna ya kuangamiza kirusi hicho. Kufumba macho kwa joho la utakaso ni kuiangamiza sanaa.
Kila jema liwashukie wadau wa safu hii. Kwa waliojeruhiwa na Pasaka kubalini hali halisi mtajipanga mwaka ujao.
Wasalaam,
KUMEKUCHA! Mzee wa Busati katumbukia kwenye buti tayari kwa mwendo wa kila Jumanne. Kwake mambo yako sawia ingawa anaelewa kwamba wapo waliopata majereha kiduchu kwenye pochi zao wakati wa ufufuo wa Bwana Yesu.
Hata hivyo, uhai ungalipo pumzi ya Mola inashuka. Hata kama mlo ni wa shida hayo ni majaribu na mapito ambayo mwenye kutoka damu sharti akumbane nayo.
Kina Momburi bila shaka sasa wanatweta hawajui watafikaje Tabata Relini. Si mchezo papake Mwanyamala hadi Tabata kwa mguu! Yataka moyo mwanawane.
Bila shaka sasa wanatembeza bakuli wakitoa sera tamu tamu ili wapate kufika tarehe njema za mwajiri. Lakini analoomba Mzee wa Busati ni kwamba msije zua misiba ambayo haipo ili mpate ngwenje za matanuzi. Mkitenda hayo mtakosa thawabu.
Juma lililopita Mwandika Busati alinena juu ya ukakasi wa sanaa hasa ya maigizo na mchezo wa ngono katika eneo hilo.
Akaweka wazi kwamba baadhi ya vikundi hivyo vya maigizo hasa vinavyoonyesha kazi zao kwenye runinga vimekuwa na mchezo mchafu wa kuwalazimisha ngono kina dada (waigizaji) ili wapate nafasi ya kuonekana kwenye vioo vya televisheni.
Na moja ya aya katika makala hayo ya juma lililopita ilisomeka hivi: “Mambo kama hayo kwa hakika yanasikitisha na kutia kichefuchefu. Kwamba kama viongozi wa vikundi fulani vya sanaa wanafikia hatua ya kudai rushwa ya ngono hii ni aibu.”
Kuanzia mwanzo wa waraka huo wa hadi mwisho hakuna pahala Mwandika Busati ametaja kikundi fulani au jina la kiongozi anayeendekeza ukware.
Lakini cha ajabu akaibuka mtu mmoja aliyejiita kiongozi wa kikundi cha sanaa za maigizo na kumtuhumu na kisha kumhukumu Mwandika Busati kwamba hakufanya kile yeye alichokiita ‘research’.
Akahitimisha hivyo kwamba katika sanaa ya maigizo mambo hayo hayapo. Mzee wa Busati naye akapata wasaa wa kuuliza iweje aitwe mdanganyifu?
Hiyo njemba ikadai eti kwa vile sikuwapa nafasi viongozi kupata maoni yao!(?). Akasisitiza hilo kwamba sikuwahoji viongozi wa makundi kisa Mzee wa Busati hakufika kwake!
Yeye ni nani hadi alazimishe kufikiwa? Pengine angesema kwamba yeye ndiye kinara wa viongozi wa vikundi vya sanaa nchini basi hoja yake ingekuwa inaelekea kwenye ukweli.
Kwani ni lazima kila kile alichokiita ‘research’ afikiwe kila mmoja? Twaangalia uwingi wa matukio na kama yeye hafanyi hivyo basi Muumba amrehemu.
Lakini ukweli wa mambo ni ule ule kwamba HAMKANI ndani ya sanaa kuna baadhi ya matukio ya kulazimisha unyumba ili binti fulani apate nafasi
Hata katika baadhi ya filamu za Kibongo nako ni kama shambiro kwa maana ya sehemu ambayo hufanyika mambo ya hovyo hasa yahusuyo ukahaba au uhuni ufananao na huo.
Mwandika Busati alitarajia kwamba jamaa aliyejiita kiongozi wa kundi la sanaa la maigizo angeleta hoja ya ushirikiano ya kukemea hali hiyo na si kushutumu na kisha kuhukumu kwamba Mwandika Busati hajui alichokinena.
Leteni hoja mezani tusemezane na si kujitakasa kwa maji ya bahari.
Haya si mashambulizi la hasha! Kinachosemwa na Mwandika Busati ni kwamba yafaa wakati mwingine kujadili ndani ya nafsi kabla ya kupayuka kwamba fulani katema urongo.
Au mpaka siku zipigwe kura za siri ndipo mpate kusadiki yasemwayo na Mzee wa Busati? Mwandika Busati aseme uwongo ili iweje?
Mlitaka asiseme ili iweje? Nanyi kuweni wadadisi na hakika mtayabaini haya kwamba yapo baadhi ya makundi ambayo hongo ya ngono imetawala.
Ndio maana juma lililopita ikawekwa wazi kwamba hawa si wasanii kwa sababu wameingia humo kiufisadi. Wamevaa joho lenye udhalimu ndani yake.
Habari ndiyo hiyo kwamba haya yasemwayo yapo na yanaendelea kufanyika. Kukaza koo na kusema kwamba fulani kasema uwongo bila shaka ni kutotenda haki.
Mzee wa Busati amefikia ukomo kwa juma hili akitaraji maoni kutoka kwa wadau.
Lakini jambo moja lililo wazi ni kwamba yu radhi hata ikibidi kupigwa mawe akitetea hoja yake. Hakuna urongo hapa. Wasanii wengi wa kike ni mashuhuda na haya.
La maana ni kuangalia namna ya kuangamiza kirusi hicho. Kufumba macho kwa joho la utakaso ni kuiangamiza sanaa.
Kila jema liwashukie wadau wa safu hii. Kwa waliojeruhiwa na Pasaka kubalini hali halisi mtajipanga mwaka ujao.
Wasalaam,
Sunday, March 16, 2008
Mwaigeuza sanaa kuwa shambiro?
Na Innocent Munyuku
KWA wajuzi wa Kiswahili, shambiro hutajwa kuwa ni sehemu ambayo hufanyika mambo ya hovyo hasa yahusuyo ukahaba au uhuni ufananao na huo.
Aghalabu shambiro huwa ni nyumba au pengine yaweza kuitwa danguro maalumu kwa kufanya umalaya.
Hilo ndilo shambiro. Wakware watajazana humo wakishindana kwa uovu wa kila aina. Hiyo ndiyo meli yao.
Mzee wa Busati juzi kasoma kwenye gazeti moja kwamba baadhi ya wasanii wa kike nchini wamekuwa wakilazimika kutoa uroda ili waonekane katika luninga.
Kwamba ili msanii wa kike apate kuonekana katika igizo fulani kupitia televisheni basi lazima avuliwe chupi.
Sharti atoe unyumba kwanza na kisha apate nafasi ya kung’ara katika igizo na mashabiki wapate kumwona akifanya vitu vyake kwenye luninga.
Mwandika Busati alipata kusikia habari ifananayo na hiyo kwamba hata katika mashindano ya kuwasaka visura rushwa ya ngono imetanda.
Mambo kama hayo kwa hakika yanasikitisha na kutia kichefuchefu. Kwamba kama viongozi wa vikundi fulani vya sanaa wanafikia hatua ya kudai rushwa ya ngono hii ni aibu.
Usanii kwa lugha nyepesi ni karama. Muumba ambaye ni Mola huwajalia baadhi yetu vipaji vya kila aina ukiwamo usanii.
Japo sanaa yahitaji pia elimu ya darasani, ukweli wa mambo ni kwamba mtu huzaliwa na sanaa.
Anachosema Mzee wa Busati ni kwamba kama leo hii watu wanatamba katika sanaa eti kwa sababu tu walitoa hongo ya ngono hawa hawawezi kuitwa wasanii.
Hawa si wasanii hata kidogo. Si wasanii kwa sababu wameingia humo kiufisadi. Wamevaa joho lenye udhalimu ndani yake. Wamelazimisha kuitwa wasanii.
Pengine yafaa waitwe makahaba au malaya ambao kwa jina la sanaa wanafanikiwa kuihadaa jamii.
Mzee wa Busati sasa amefumbua macho na anachokiona ni historia chafu ya viongozi wa vikundi vya sanaa na wasanii wao.
Kama kiongozi anathubutu kutaka mapenzi kwa msanii wa kike ili apewe kipaumbele ni lini basi kaya zetu zitawaona wasanii wa kweli?
Dunia ya aina hii haiwezi kukubalika iendelee kutamba chini ya jua. Hawa hapa si pahala pao. Yafaa waangamizwe ili watoweke.
Haifai kuwa na wasanii ambao historia zao ni mbaya. Haifai kuwa na waigizaji wanaowika kwa sababu walitoa miili yao kama asusa kwa viongozi wao wa sanaa.
Hawa ndio wanaotarajiwa kuwa vinara wa kupinga maovu kwa kutumia vipaji vyao. Hawa ndio dira ya jamii. Kama wanakiuka maadili basi si vema kuwaita wasanii bali wahuni!
Katika hili Mzee wa Busati anawaomba wadau kuungana ili kupiga vita maovu kama hayo. Mambo ya aina hii si ya kuyafumbia macho kwani mwisho wake ni mbaya.
Hawa wanatarajiwa kuwa wahamasishaji wa mambo mbalimbali kama vile vita dhidi ya Ukimwi au ufisadi.
Leo hii msanii atawezaje kupanda jukwaani kuhamasisha vita dhidi ya Ukimwi huku akiwa mkware? Bila shaka atakuwa anacheza muziki asioujua.
Basi na wenye masikio wasikie maneno haya ambayo Mwandika Busati ananena kwa uwazi na ukweli. Wanawali fungeni vibwebwe kupinga mtindo wa kutoa miili yenu kwa ajili ya kuonekana katika televisheni.
Enendeni kila njia mseme kwamba sasa inatosha na si wakati wa kuendelea kunyanyasika kwa jina la sanaa.
Kama baadhi yenu mnadhani haiwezekani kupinga udhalilishwaji huo basi badilisheni fani. Jihalalisheni moja kwa moja kuwa makahaba kwani madanguro yangalipo.
Mzee wa Busati amefikia ukomo kwa juma hili ambalo waumini wa Kristo wanasubiri ufufuo wake.
Kila jema katika Pasaka ila angalieni msije angusha magari kama ilivyo desturi ya Mzee wa Kutibua anayetamba kifedhuli maeneo ya Makumbusho. Msifuate nyayo zake kwani huko ni kujiangamiza.
Wasalaam,
KWA wajuzi wa Kiswahili, shambiro hutajwa kuwa ni sehemu ambayo hufanyika mambo ya hovyo hasa yahusuyo ukahaba au uhuni ufananao na huo.
Aghalabu shambiro huwa ni nyumba au pengine yaweza kuitwa danguro maalumu kwa kufanya umalaya.
Hilo ndilo shambiro. Wakware watajazana humo wakishindana kwa uovu wa kila aina. Hiyo ndiyo meli yao.
Mzee wa Busati juzi kasoma kwenye gazeti moja kwamba baadhi ya wasanii wa kike nchini wamekuwa wakilazimika kutoa uroda ili waonekane katika luninga.
Kwamba ili msanii wa kike apate kuonekana katika igizo fulani kupitia televisheni basi lazima avuliwe chupi.
Sharti atoe unyumba kwanza na kisha apate nafasi ya kung’ara katika igizo na mashabiki wapate kumwona akifanya vitu vyake kwenye luninga.
Mwandika Busati alipata kusikia habari ifananayo na hiyo kwamba hata katika mashindano ya kuwasaka visura rushwa ya ngono imetanda.
Mambo kama hayo kwa hakika yanasikitisha na kutia kichefuchefu. Kwamba kama viongozi wa vikundi fulani vya sanaa wanafikia hatua ya kudai rushwa ya ngono hii ni aibu.
Usanii kwa lugha nyepesi ni karama. Muumba ambaye ni Mola huwajalia baadhi yetu vipaji vya kila aina ukiwamo usanii.
Japo sanaa yahitaji pia elimu ya darasani, ukweli wa mambo ni kwamba mtu huzaliwa na sanaa.
Anachosema Mzee wa Busati ni kwamba kama leo hii watu wanatamba katika sanaa eti kwa sababu tu walitoa hongo ya ngono hawa hawawezi kuitwa wasanii.
Hawa si wasanii hata kidogo. Si wasanii kwa sababu wameingia humo kiufisadi. Wamevaa joho lenye udhalimu ndani yake. Wamelazimisha kuitwa wasanii.
Pengine yafaa waitwe makahaba au malaya ambao kwa jina la sanaa wanafanikiwa kuihadaa jamii.
Mzee wa Busati sasa amefumbua macho na anachokiona ni historia chafu ya viongozi wa vikundi vya sanaa na wasanii wao.
Kama kiongozi anathubutu kutaka mapenzi kwa msanii wa kike ili apewe kipaumbele ni lini basi kaya zetu zitawaona wasanii wa kweli?
Dunia ya aina hii haiwezi kukubalika iendelee kutamba chini ya jua. Hawa hapa si pahala pao. Yafaa waangamizwe ili watoweke.
Haifai kuwa na wasanii ambao historia zao ni mbaya. Haifai kuwa na waigizaji wanaowika kwa sababu walitoa miili yao kama asusa kwa viongozi wao wa sanaa.
Hawa ndio wanaotarajiwa kuwa vinara wa kupinga maovu kwa kutumia vipaji vyao. Hawa ndio dira ya jamii. Kama wanakiuka maadili basi si vema kuwaita wasanii bali wahuni!
Katika hili Mzee wa Busati anawaomba wadau kuungana ili kupiga vita maovu kama hayo. Mambo ya aina hii si ya kuyafumbia macho kwani mwisho wake ni mbaya.
Hawa wanatarajiwa kuwa wahamasishaji wa mambo mbalimbali kama vile vita dhidi ya Ukimwi au ufisadi.
Leo hii msanii atawezaje kupanda jukwaani kuhamasisha vita dhidi ya Ukimwi huku akiwa mkware? Bila shaka atakuwa anacheza muziki asioujua.
Basi na wenye masikio wasikie maneno haya ambayo Mwandika Busati ananena kwa uwazi na ukweli. Wanawali fungeni vibwebwe kupinga mtindo wa kutoa miili yenu kwa ajili ya kuonekana katika televisheni.
Enendeni kila njia mseme kwamba sasa inatosha na si wakati wa kuendelea kunyanyasika kwa jina la sanaa.
Kama baadhi yenu mnadhani haiwezekani kupinga udhalilishwaji huo basi badilisheni fani. Jihalalisheni moja kwa moja kuwa makahaba kwani madanguro yangalipo.
Mzee wa Busati amefikia ukomo kwa juma hili ambalo waumini wa Kristo wanasubiri ufufuo wake.
Kila jema katika Pasaka ila angalieni msije angusha magari kama ilivyo desturi ya Mzee wa Kutibua anayetamba kifedhuli maeneo ya Makumbusho. Msifuate nyayo zake kwani huko ni kujiangamiza.
Wasalaam,
Subscribe to:
Posts (Atom)