Na Innocent Munyuku
LEO ni matumbo joto. Wadanganyika wamekuwa wenye uchu wa kutaka kufahamu utamu au shubiri ya bajeti kwa mwaka huu wa fedha.
Walalahoi ambao kimsingi ndio wenye kwenye nnji hii walishamaliza utabiri wao kwa hitimisho kwamba mwaka huu hakuna unafuu. Wataendelea kusaga meno kwa makali ya maisha.
Mzee wa Busati anachokiona ni kwamba kama utabiri wa walalahoi utakuwa wa kweli basi kazi kubwa ipo. Tujiandae kuwa na ongezeko la vibaka mitaani ambao kwao hiyo ndiyo njia pekee ya kujikwamua kimaisha.
Huo ulikuwa utangulizi kwa Mwandika Busati ambaye leo hii anajutia wema wake kwa watu wa Kibosho. Naam lazima ajute kwani kile kijamaa kinachojiita Mzee wa Kutibua kaonyeshwa mji na sasa anaanza kutusi wajanja wake.
Kwa hakika anachefua kama ilivyo Taifa Stars ambayo sasa ni kama inatembea gizani pasipo na dira inayoeleweka. Enewei huyu atapatiwa dawa muda si mrefu na hakika kilimilimi chake kinafikia ukingo.
Kilichomleta Mzee wa Busati hapa leo ni kilio chake kwa Taifa Stars ambayo juzi imenyukwa bao 1-0 na Cape Verde katika mchezo wa pili wa kuwania nafasi ya kucheza Kombe la Dunia mwaka 2010.
Si utani kwa sasa Wabongo wengi wametumbukia nyongo. Ukipita vijiweni hadithi ni juu ya ubutu wa safu ya ushambuliaji. Wanalalama hadi koo zao kukauka. Wanayo haki ya kulalama kwani wanadhani kuna pahala kocha ameteleza.
Wengine wanasema mpira wa kibongo ulisharogwa tangu enzi zileeeeee. Kwa hiyo ni kama mwendelezo wa nuksi dimbani. Kila wanapojaribu kufurukuta holaa.
Cape Verde wanachekelea kwa ushindi wao mlaini. Manake ilikuwa kama zali la mentali. Mwishoni mwa wiki si ajabu Taifa Stars ikafanywa mbuzi wa shughuli kwenye Uwanja wa Taifa Darisalama.
Mwandika Busati anasema hayo kwa sababu anaamini mechi kati ya Stars na Cameroon ni ngumu kwa upande wa watoto wa Maximo. Tuombe Mungu wakali wanaofanana na Eto’o wasiingie dimbani.
TMK Halisi wao wamekuja na Tatu Bila lakini kwa hili tifu la Cameroon na Stars si ajabu zikawa saba bila. Tusubiri tuone.
Mambo mengine yanachanganya kichwa kwa sababu haiwezekani kila mwaka bongo ndio iwe kichwa cha kujifunzia kunyolea. Hivi ni kweli soka hii imerogwa?
Kwa mechi ya keshokutwa la maana linaloweza kufanywa ni kuamini katika hadithi ya kwenye Biblia kuhusu Daudi na Goliath. Kwamba tusubiri miujiza la kuiangusha Cameroon kwa kombeo kama alivyofanya Daudi kwa Goliath.
Vinginevyo hali itakuwa ya kuchukiza kwa sababu Cameroon hawataki utani dimbani. Nani asiyejua uhodari wao? Kama kuna mwenye shaka na soka ya watu hao basi ana lake jambo.
Mzee wa Busati si mara moja au mbili ameshaweka wazi misimamo yake kwamba kwa soka hii ya kwetu ni heri tuangalie njia mbadala kuliko staili ya kanyaga twende.
Hivi kuna raha gani ya kuingia mashindanoni kila msimu na kutoka kapa? Kwanini taifa likubali kuwa msukule wa soka? Lazima kuwe na mwamko mpya sasa!
Mwandika Busati ameona aanze na hilo kwa sababu limekuwa likimkera kila siku. Wadau waje na programu endelevu ili siku moja Tanzania ing’are katika soka duniani.
Wakati mwingine Mzee wa Busati huwa anawaza na kuwazua kwamba Wabongo waliumbwa kwa ajili ya kuumbuka kwenye michezo? Hivi ndivyo ilivyo?
Bila shaka sivyo ila ukweli ni kwamba watangulizi katika mamlaka ya soka kuna pahala walikosea. Walikosea kwa kuendekeza soga na malumbano na vinara wa Serikali.
Walikosea kwa kuhubiri falsafa ya soka fitna badala ya kuweka wazi programu za maana katika maendeleo ya soka. Muda mwingi ulitumika kusuguana na kulumbana.
Mwandika Busati anakaribia kufikia ukingoni kwa juma hili. Husemwa kwamba jambo jema maishani ni kuandaa mambo kabla ya umauti. Kama ni wosia yafaa uandikwe mapema ili kila kitu kiwe sawia.
Basi Mzee wa Busati ameanza kuandika wosia kwa wadau wake. Mkiona amezimika ghafla mjue kwamba kila kilicho chenu kitaendelea kuwa mikononi mwenu. Ukweli ni kwamba angetamani apate wasaa wa kufufuka siku ya tatu lakini hilo haliwezekani.
Vinginevyo, kaeni na amani ya Mola. Pendaneni na kwa umoja wenu hakuna atakayethubutu kuwaangusha.
Wasalaam,
Monday, June 9, 2008
Subscribe to:
Posts (Atom)